Thursday, April 16, 2020

UHAKIKI WA RIWAYA YA WATOTO WA MAMA N'TILIE


RIWAYA:WATOTO WA MAMA NTILIE
MWANDISHI: EMMANUEL MBOGO
WACHAPISHAJI: HEKO PUBLISHERS
MWAKA: 2002
WASIFU WA MWANDISHI
Emmanuel Mbogo ni Profesa wa drama na fasihi na amehudumu katika vyuo vikuu mbalimbali ikiwemo, Chuo Kikuu cha Kenyatta Kenya na Chuo Kikuu Huria. Mbogo ni mwanafasihi mahiri sana katika Afrika ya Mashariki.
MUHTASARI WA RIWAYA
Maman’tilie, mama mwenye watoto wawili lakini wote wamefukuzwa shule kwa kukosa ada na sare. Anajitahidi hapa na pale ili apate, lakini wapi? Pesa imegeuka nyoka inateleza kwenye nyasi. Mumewe Mzee Lomolomo hana muda, yeye kila kukuchapo huelekea bunge la walevi kunywa pombe tani yake. Akiwa huko hunywa na kurudi nyumbani akiwa mbwii! Mwisho mwandishi anauliza swali gumu, ‘Nani anajali?’
MAUDHUI
Maudhui hujumuisha mawazo na pengine mafunzo mbalimbali yaliyomsukuma mtunzi ama mwandishi wa kazi ya fasihi akaandika kazi yake.
DHAMIRA
Dhamira ni lile wazo linalomfanya mwandishi wa kazi ya fasihi aandike kazi yake. Katika riwaya hii, dhamira nyingi zimejadiliwa kama:
UMASIKINI
Dhamira hii imetawala katika riwaya. Asilimia kubwa ya wahusika ni watu wenye maisha ya dhiki na kazi za kijungujiko. Umasikini wao unadhihirishwa na mitaa wanayoishi kama: Manzese, Msufini, Tabata, Kisutu na Temeke. Maeneo haya ndiyo yaitwayo uswahilini leo hii.
Zita na Pita wanafukuzwa shule kwa sababu ya kukosa ada na sare (uk 1). Mamant’ilie naye anatumia maji ya mwarobaini kutibu homa yake kwa sababu hana pesa ya kununulia dawa za hospitali.
ULEVI
Unywaji wa pombe kupitiliza huweza kusababisha madhara makubwa kwa mtumiaji. Mzee Lomolomo ni mlevi mzoefu, kutokana na ulevi wake, anashindwa hata kuwalipia ada wanae ili waendelee na shule. Ni ulevi huohuo unamfanya aishi maisha ya dhiki huku akishindwa kutoa mchango kwa familia yake na taifa linalomtegemea. Mwisho Lomolomo anakufa kwa sababu ya pombe.
Mwandishi anasema, “… Lomolomo alikuwa lofa, mtu wa kazi za kijungujiko na vipesa vyake viliishia kwenye pombe…” (uk 7).
MALEZI YA WATOTO
Watoto wasipopata malezi yanayostahili kutoka kwa wazazi wote wawili huwa ni rahisi kwao kujiingiza katika mambo yasiyofaa.
Mwandishi anaonyesha aina tatu za watoto. Kwanza kuna Zita na Pita. Hawa wana wazazi wote wawili lakini baba hajishughulishi na malezi yao. Pia mama naye ametingwa na shughuli nyingi katika genge lake la uuzaji wa chakula. Zita na Pita hawana malezi ya kueleweka. Hali hii inamfanya Pita ajiingize katika biashara ya madawa ya kulevya.
Pili, kuna Dan na Musa hawa hawana baba, wanaishi na mama zao tu. Mama zao hawawajali wala kuwakemea kwa chochote kibaya wanachofanya. Dan anajiingiza katika ujambazi na kupoteza maisha. Musa anajiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya na kuishia jela.
Tatu kuna Kurwa na Doto. Hawa hawana wazazi kabisa. mwandishi anasema, “… walikuwa chokoraa namba moja, kupigana kulala na njaa, kukamatwa na polisi… yalikuwa sehemu ya maisha yao…”
Doto anajiingiza katika ujambazi, huko anauawa na mlinzi Simango.
RUSHWA
Rushwa imeota mizizi katika jamii. Kila uendako, kila upitako na kila utokako utaambiwa toa rushwa ili upate kitu fulani.
Mamant’ilie alishindwa kuyamudu maisha ya mjini kwa sababu ya rushwa aliyokuwa akiwapa askari wa jiji. Kwa kalamu yake isiyoisha wino, Mbogo anaandika, “KSodi na hongo kwa askari wa jiji, ziliikamua faida yake.” (uk 32).
MMOMONYOKO WA MAADILI 
Maadili ya siku hizi si yale ya zamani. Miaka inabadilika na vizazi navyo vinabadilika. Watu ni watu tu lakini hawana utu. Watoto wadogo sasa wanavuta sigara na kutafuna mirungi kama tumuonavyo Dan na Musa. Watu hawana moyo wa kusaidiana tena, wao wanaamini kuwa kila mwenye janga atalila peke yake. Zita anazidiwa na maradhi yaliyosababishwa na kuumwa na mbwa mwenye kichaa. Watu hawakumsaidia, badala yake walivishangilia vioja alivyovifanya. Mwandishi anatuonesha Zenabu akiwaomba msaada na kuwakalipia, “Nisaidieni, mnacheka nini? Wendawazimu wakubwa.” (uk 82).
NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII
Nafasi ya mwanamke ni jumla ya matendo yote yafanywayo na mwanamke katika jamii yake. Mara nyingi huwa mabaya na yenye mtazamo hasi, lakini mara chache huwa mazuri yenye mtazamo chanya. Mwandishi wa riwaya hii, amemchora na kumjadili mwanamke kwa mawanda mapana kama inavyoelezwa:
  • Mama mlezi na mwangalizi mkuu wa familia. Maman’tilie ndiye aliyejua familia yake ile nini, ifanye nini na iishi vipi. Mumewe mzee Lomolomo hakuwa na mchango wowote. Yeye kila kukuchapo alikwenda kilingeni kufakamia mataputapu na pombe haramu.
  • Mwenye huruma na moyo  wa kutoa msaada. Zenabu anawakilisha tabia hii. Alimsaidia Pita alipokuwa na njaa. Ni yeye akishirikiana na Mama sara walimpeleka Zita hospitali.
  • Mwenye mapenzi na kazi. Kurwa anapenda kazi, alifuatana na Maman’tilie kwenda gengeni, huko alimsaidia kuuza chakula. Hata siku moja kurwa hakuchoka kufanya kazi.
  • Aliyenyimwa elimu. Zita ni mwanamke aliyenyimwa elimu. Anafukuzwa shule kwa kukosa ada na sare.
  • Mzembe na asiyejali malezi ya watoto. Mama Musa ni mzembe na hajali malezi ya mwanae. Yeye ameshika themanini zake na Musa kashika hamsini zake.

UJUMBE
Ujumbe ni funzo litolewalo na kazi ya fasihi. Mafunzo mengi yametolewa katika riwaya hii:
  • Watoto wasifukuzwe shule kwa sababu ya kukosa ada, kwani kufanya hivyo kunawanyima haki yao ya kupata elimu.
  • Majalala ya kuchoma takataka yajengwe mbali na makazi ya watu. Mwandishi anasema, “Mapafu ya wakazi yaliendelea kuteketea kwa moshi siku hadi siku… watu wale walikuwa wanakufa taratibu.” (uk 27).
  • Pombe si suluhisho la matatizo.
  • Mzaha mzaha hutumbua usaha. Zita alikwaruzwa na mbwa mwenye kichaa, lakini wakapuuzia, mwishi ni kifo cha Zita.

MIGOGORO
Migogoro ni kukosekana kwa maelewano baina ya watu binafsi, jamii, taifa au mataifa. Migogoro iliyojitokeza ni:
Migogoro ya wahusika
  • Mwalimu Chikoya na wanafunzi wasiokuwa na ada wala sare za shule. Huu unasababishwa na wanafunzi wasiokuwa na ada wala sare. Suluhisho lake ni wanafunzi hao kufukuzwa shule.
  • Maman’tilie na mzee Lomolomo. Huu unasababishwa na ulevi wa Lomolomo. Suluhisho ni kifo cha mzee Lomolomo.
  • Peter na Doto. Huu unasababishwa na Doto kumfukuza Pita jaani. Suluhisho la mgogoro huu ni Kurwa kumsaidia Peter.
  • Mgogoro wa nafsi, Huu unampata Peter, yeye anamawazo ya kurudi shule lakini hajui ni kipi afanye ili apate pesa za kumrudisha.
  • Migogoro mingine ni: migogoro ya kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na kijamii.

FALSAFA
Falsafa ni imani ya mwandishi. Emmanuel Mbogo anaamini kuwasaidia watoto kupata elimu yao kutaondoa matatizo yanayozuia ujenzi wa jamii mpya.
MTAZAMO/MSIMAMO
Mwandishi anamsimamo wa kimapinduzi. Anaamini kuwapatia watoto elimu na kusimamia malezi yao kutaliokoa taifa.
UCHAMBUZI WA FANI NA VIPENGELE VYAKE
Fani ni ule ufundi wa kisanaa anaoutumia msanii katika kazi yake. Fani ndiyo hutupatia kile kiitwacho maudhui. Katia riwaya hii, fani imechambuliwa Kama ifuatavyo:
WAHUSIKA
Wahusika ni watu au viumbe waliokusudiwa uwakilisha tabia za watu katika kazi ya fasihi. Wahusika waliopo katika riwaya hii ni:
Maman’tilie. 
Ni mke wa mzee Lomolomo. Ni mchapakazi. Ni mama yao Zita na Peter na anafaa kuigwa na jamii.
Lomolomo. 
Ni mume wa Maman’tilie. Ni mlevi wa pombe haramu. Hawajibiki katika malezi ya watoto wake na hafai kuigwa na jamii.
Zita. 
Mtoto wa Maman’tilie na mzee Lomolomo. Alifukuzwa shule kwa kukosa ada na sare akiwa darasa la sita. Pia, alikwaruzwa na mbwa mwenye kichaa. Mwisho anakufa kwa kupuuzia ule mkwaruzo wa mbwa.
Peter. 
Mtoto wa Mzee Lomolomo na Maman’tilie. Anafukuzwa shule akiwa darasa la tano. Anatafuta ridhiki dampo. Baadaye anajiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya.
Chikoya.
 Ni mwalimu mkuu wa shule ya msingi Makurumla. Anawafukuza wanafunzi wasiokuwa na sare wala ada.
Musa.
 Anafukuzwa shule kwa kukosa ada na sare. Hamheshimu mama yake. Anajiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya.
Sara. 
Mwanafunzi wa Makurumla na ni jirani yao Zita.
Mama Sara. 
Mama yake Sara. Alimsaidia Zita alipopatwa na kichaa.
Zenabu. 
Anafanya kazi Kikale Bar. Ana huruma. Anafaa kuigwa.
Kurwa. 
Ni yatima. Anaishi vichochoroni. Anategemea chakula cha dampo. Anasingiziwa kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya.
Doto. 
Ni yatima. Anauawa kwa kujihusisha na ujambazi.
Rhemtulah. 
Ni mfanyabiashara wa kihindi.
Simango. 
Ni mlinzi wa Rhemtulah. Anawaua Doto na Dan.
Dani. 
Ni mtoto ambaye hamjui baba yake. Anauawa kwa kujihusisha na ujambazi.
Jane.
 Aliwalea Doto na Kurwa baada ya kufiwa na mama yao. Naye pia anakufa.
Master Baroni. 
Anawatumia watoto katika biashara yake ya madawa ya kulevya. Si mfano wa kuigwa na jamii.
MATUMIZI YA LUGHA
Fasihi ni sanaa itoayo maudhui kwa kutumia lugha ya maneno ambayo hutamkwa au kuandiwa. Kipengele cha lugha ni muhimu kwani ndicho kinachotofautisha fasihi na sanaa zingine.
Lugha iliyotumika katika riwaya hii ni nyepesi na yenye kueleweka. Mwandishi ametumia vipengele vingi vipatikanavyo katika matumizi ya lugha kama: ucheshi na lugha ya picha, misemo na tamathali za semi.
TAMATHALI ZA SEMI
Tamathali za semi ni maneno au sentensi ambazo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia nguvu katika maana, mtindo na hata sauti katika maandishi ama kusema. Wakati mwingine hutumiwa ili kupamba na kuongeza utamu wa kazi za fasihi. Mwandishi ametumia tamathali nyingi za semi kama:
Tanakali sauti (onomatopoeia). 
Tanakali sauti ni maneno au nomino ziundwazo katika sentensi kutokana na sauti zinazofanana.
            “Bwee!”
           “Paah!” (uk. 5)
Tashibiha. 
Katika tamathali hii, watu ama vitu viwili au zaidi hulinganishwa na watu au vitu vingine kwa kutumia maneno, ‘kama’, ‘mithili’…
        “Masikio yamesimama wima kama anasisitiza kitu.” (uk. 2)
         “Mdomo wake uliokaa kama bakuli la pombe.” (uk. 10)
Tafsida. 
Hii hutumika kupunguza ukali wa maneno.
         “Akaenda haja ndogo.” (uk. 2)
        “Akakitibu kidonda chake kwa maji ya chumvichumvi.” (uk 55)
Takriri. 
tamathali hii, maneno hurudiwarudiwa ili kuonyesha msisitizo.
         “Yalaa! Yalaa!” (uk 2)
          “Mjomba! Mjomba!”
Mdokezo. 
Hapa msemaji husema kitu bila kukimalizia kukitaja.
       “Shikamoo mama…” (uk 6)
        “Una… una…” (uk 11)
 Tashihisi. 
Hapa vitu hupewa sifa alizonazo binadamu.
         “Maman’tilie alimtupia jicho bintie.”
         “Mabega yameangalia juu.” (uk 10).
Mjalizo.
 Katika tamathali hii maneno hufuatana pasipo kiunganishi.
         “Walikaa, wakala, wakanywa maji, wakamshukuru Mungu.”
Kejeli. 
Hii ni tamathali ya semi ambayo maneno yake huwa kinyume na maana yanayotoa.
          “Naye pita aliitikia salamu hizo za ukarimu kwa kupiga chafya             mbili au tatu.” (uk 19).
          “Lomolomo uso wake uliopendeza kwa chang’aa…” (uk 70).
Sitiari. 
Tamathali hii hulinganisha vitu bila kutumia viunganishi.
“Wakatembea mwendo wa farasi.” (uk 86).
Ritifaa.
 Katika tamathali hii, mtu huongea na kitu ambacho husikika kwa fikra tu.
“Kumbe wewe na mwanao mna hila kiasi hiki? Mmepatana kuondoka na kusafiri katika dau moja.” (uk 94).
Misemo.
“Ukienda Tabata utapata.”
“Waswahili hawana dogo.”
Matumizi ya lugha za kigeni.
“Nikukonekti.” (uk 78).
Methali.
“Kamba hukatikia pembamba.”
Ucheshi na lugha ya picha.
“Alikunywa funda moja, akajisikilizia kabla ya kulimeza. Alisikia pombe ikisafiri kufuata barabara ya lami hadi tumboni.” (uk 87).
MTINDO
Mtindo ni ule upekee wa mtunzi wakazi ya fasihi na mtunzi mwingine. Mfano, mwandishi anaweza kutumia, nyimbo, mashairi, nafsi zote, dayolojia, monolojia n.k. mwandishi amefanikisha mtindo wake kwa kutumia,
Matumizi ya nyimbo. 
Mfano katika ukurasa wa 10 Lomolomo aliimba,
“Kuleni nae,
Hata bangi vuteni nae,
Lakini ni bure,
Mwenzenu nimezaa naye…”
Mwandishi katumia monolojia (masimulizi) na dayolojia (majibishano).
Mwandishi katumia nafsi zote tatu.
MUUNDO
Riwaya hii imetumia muundo wa kurukia. Mwandishi amemuonyesha Lomolomo akiwa katika hali ya ulevi, baadaye anatukumbusha alipokuwa anafanya kazi bandarini. Vilevile anawaonyesha Kurwa na Doto wakiishi peke yao. Lakini baadaye anatukumbusha kipindi walipokuwa wanalelewa na mama yao ambaye hata hivyo alifariki kisha wakalelewa na Jane ambaye naye anafariki.
MANDHARI
Mandhari ni sehemu ambayo kazi ya fasihi hutendeka. Riwaya hii imetumia mandhari ya jiji la Dar es Salaam na mitaa yake kama, Manzese, Msufini, Tabata, Kisutu, Urafiki na mtaa wa Ajentina.
JINA LA KITABU
Jina la kitabu, Watoto wa Maman’tilie, linasadifu yaliyomo, kwani ndani ya riwaya hii kuna mhusika mkuu ambaye ndiye Maman’tilie.
Riwaya hii inamwonesha mama huyu akijaribu kujinasua yeye na watoto wake katika wimbi la umasikini, lakini wapi? Jitihada zote anazofanya zinagonga mwamba na matatizo yake yanazidi kuongezeka.
KUFAULU KIMAUDHUI
Mwandishi amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuonyesha shida wazipatazo watoto wa mitaani.
Mwandishi amefanikiwa kuonyesha madhara ya umasikini.
Mwandishi ameonyesha madhara ya unywaji wa pombe kupita kiasi na ulevi.

KUFAULU KIFANI
Amekitendea haki kipengele cha mtindo, kwani humo ametumia vipengele vingi kama nyimbo n.k.
Kazi yake imeshibishwa kwa tamathali nyingi za semi.
Ametumia lugha ya picha inayomwelewesha zaidi msomaji.
KUTOFAULU KWA MWANDISHI
1. Kimaudhui. Mtazamo wa mwandishi katika suala la umasikini hauko sawa. Yeye anaamini hata ukifanya kazi kwa bidii kama ni masikini utaendelea kuwa masikini kama tumuonavyo Maman’tilie.
2. Kifani wahusika wa mwandishi hawana uwiano. Wengi wao ni watu masikini. Pia, mandhari yote yaliyotumiwa na mwandishi ni ya mjini. Mwandishi ameutenga upande wa kijijini ambao nao kama ungetazamwa, jamii ingejifunza mengi.

UHAKIKI WA DIWANI YA WASAKATONGE


DIWANI :WASAKATONGE
MWANDISHI: MUHAMMED SEIF KHATIBU
MCHAPISHAJI: OXFORD UNIVERSITY PRESS
MWAKA: 2003
UTANGULIZI
Diwani ya Wasakatonge ni miongoni mwa diwani za hivi karibuni zinazotanabaisha matatizo mbalimbali yanayoikumba jamii katika maisha yake ya kila siku. Matatizo hayo yanaonekana kuwa kama saratani isiyo na tiba. Hata hivyo, msanii ana matumaini kwamba, iwapo wananchi wa kawaida wataungana na kuamua kupambana, ni dhahiri kwamba matatizo hayo yatatoweka kabisa. Miongoni mwa matatizo hayo yataoneshwa kwenye kipengele cha maudhui huku yakishadidiwa na fani.
DHAMIRA: 
Ni jumla ya maana anayovumbua mwandishi aandikapo kazi yake na jumla ya maana anayoipata msomaji pindi anapoisoma kazi fulani ya kifasihi. Kifasihi kuna aina mbili za dhamira yaani dhamira kuu na dhamira ndogondogo. Dhamira kuu ni lile wazo kuu la mwandishi katika kazi, wakati dhamira ndogondogo ni zile dhamira zinazojitokeza ili kuipa nguvu dhamira kuu. Dhamira zilizojitokeza katika diwani hii ni kama ifuatavyo:
UONGOZI MBAYA: 
Jamii nyingi za kiafrika zinakabiliwa na suala la uongozi mbaya. Wapo viongozi ambao hawataki kuachia madaraka kama ilivyooneshwa katika shairi la “MADIKTETA”
"Mizinga nayo mitutu,
Haitoi risasi,
Hutoa marais,
Walio madikteta"
Ni kweli kuwa viongozi madikteta ndio chanzo cha kukosekana kwa maendeleo katika bara la afrika.
MATABAKA
Migogoro mingi inaibuka katika jamii kati ya tabaka la wenye nacho na tabaka la wasionacho katika kugombea mahitaji ya kila siku. Mfano katika shairi la "TONGE LA UGALI"
Wanapigana
Wanaumizana,
Wanauwana,
Kwa tonge la ugali!”
Tunaoneshwa kuwa tabaka masikini linajaribu kupambana na tabaka la tajiri ili liweze kupata tonge la ugali.
UMASIKINI 
Mshairi amejadili kwa kina kuhusu tatizo la umaskini katika shairi la WASAKATONGE anaonyesha  jinsi ambavyo masikini wanavyotokwa jasho kwa sababu ya kufanya kazi ngumu zenye mishahara ya kijungujiko. 
"Jua kali na wasakatonge,
Wao ni manamba,
Mashambani,
Ni wachapakazi viwandani,
Lakini bado ni masikini."
Wasakatonge wanafanya kila jitihada ili waweze kujinasua  kutoka  katika umasikini lakini inashindikana na jasho linaendelea kuwatoka.
MMOMONYOKO WA MAADILI
Dhamira hii imejadili katika shairi la JIWE SI MCHI. Mshairi amekemea tabia ya wanawake wanaooana wao wenyewe kana kwamba wanaume wamekwisha. Mshairi anayalaani mambo haya mapya yanaingilia taratibu na kutaka kuharibu tamaduni zetu za kiafrika  
UKOLONI MAMBO LEO
Hali hii hutufanya tuwe watumwa wa ukoloni mamboleo baada ya kuondokana na ukoloni mkongwe. Katika shairi la “BUNDI” (uk.43) tunaambiwa kuwa uhuru wetu tulioupata hatujaufaidi hata kidogo kutokana na kupigwa nyundo ya kichwa na ukoloni mamboleo. Ukoloni huu ambao umefanikishwa na Bundi, tunaambiwa kuwa uko nasi kila kukicha. Ukoloni mamboleo ni mfumo usio na usawa hata kidogo. Ni mfumo ambao unawafanya wanyonge waendelee kuwa masikini, wasiomithilika huku matajiri wakiendelea kuwa watu wenye mali kupindukia. Haya yote tunayapata katika shairi la “KLABU” (uk.50) juu ya ukoloni mamboleo kwa kutuasa tuchapekazi, tujenge viwanda, tuboreshe kilimo na ufugaji, tuinue elimu, kukuza uchumi na tupige vita rushwa.
UNAFIKI:
 Katika diwani hii tunaambiwa kuwa baadhi yetu hasa wanasiasa, viongozi au wananchi ni wanafiki wakubwa. Kwani kitendo cha baadhi ya watu kujiona kuwa hawana dhambi ni cha kinafiki kwa sababu, hakuna mwanadamu asiye na dhambi kama shairi la “WASO DHAMBI” (uk.1) linavyosema;
Wavilemba!
Wavilemba, na majoho, tasibihi,
Wajigamba, safi ni roho, ni kebehe,
Wanotenda,
Unafiki.
Unafiki mwingine unajionesha katika siasa ambapo baadhi ya viongozi hupata uongozi kwa kujipendekeza na kutoa maneno ya hapa na pale kwa wale wanawapatia hivyo vyeo. Haya tunayapata katika shairi la “WARAMBA NYAYO” (uk.46-47)
‘Wajikomba,
Ili kupata vyeo,
Na uluwa.”
USALITI: 
Mshairi Mohammed Seif Khatibu ameonesha suala la usaliti katika diwani hii  ya WASAKATONGE, kwani tunaambiwa kuwa, mara nyingi tunakuwa pamoja katika safari ya kutafuta kitu fulani lakini pindi kinapopatikana tu tunawatenga baadhi ya watafutaji wenzetu. Haya yanadhihirishwa wazi katika shairi la “SIKULIWA SIKUZAMA” (uk.22-23) ambapo msanii anabainisha kwa kusema kuwa;
Nilitoswa baharini,
Ya dharuba na tufani,
Walitaka nizame,
Wao wanitazame,
Nife maji wakiona,
Waangue na vicheko,
Na kushangilia,
Ushindi wao!”
MAPENZI/MAHABA
Kwa vile mshairi huyu anaona kuwa mapenzi ndicho kitu cha thamani kubwa kwake ayakosapo au amkosapo yule ampendaye hukonda na kudhoofika mwili kama asemavyo katika shairi la “SILI NIKASHIBA” (uk.17)
“Sili nikashiba, nikikukumbuka,
Hula haba, na kushikashika,
Ni chozi za huba, kweli nasumbuka.

UJUMBE
  1. Uongozi mbaya ndiyo chanzo cha kukosekana Kwa maendeleo katika Bara la afrika. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la MADIKTETA.
  2. Uhusiano wa unyonyaji umesababisha matabaka na masikini ndiye anayeumia. Haya yamejadiliwa katika shairi la TONGE LA UGALI.
  3. Umasikini Ni tatizo sugu katika jamii. Shairi la WASAKATONGE
  4. Viongozi wengi hubadilika Kama vinyonga hivyo katika uchaguzi wapiga Kura wawe makini. Katika shairi la VINYONGA

MSIMAMO
Mwandishi ana msimamo wa kimapinduzi anashauri kuwa, ili kuondoa matatizo yanayojitokeza katika jamii lazima jamii ifuate misingi ya usawa na haki.
FALSAFA 
Mwandishi anaamini kuwa jamii yenye maendeleo ni ile inayofuata misingi ya haki na usawa.
FANI
MUUNDO
Mwandishi ametumia miundo hii:
Tathlitha 
Ni muundo ambao ubeti mmoja huwa na mistari mitatu. Mfano wa mashairi yaliyotumia muundo huu ni “Nilinde”, “Tutabakia wawili”, “Itoe kauli yako”, “usiku wa kiza” na “Sikujua”.
Tarbia
Ni muundo unaotumia mistari minne. Na n i muundo unaopendwa kutumiwa na washairi wengi.Mfano wa mashairi yaliyotumia muundo huu ni “Mahaba”, “Machozi ya dhiki”, “Mcheza hawi kiwete”, “Sivui maji mafu”
Sabilia
Muundo huu hutumia zaidi ya mistari sita na kuendeleaka katika beti. Mfano ni mashairi ya “Waso dhambi”, “Sikuliwa sikuzama”, “Madikteta”, “Si wewe?”, “Vinyonga”
MTINDO
Mwandishi ametumia mitindo yote miwili: mtindo wa kimapokeo na mtindo wa kisasa.
Baadhi ya mashairi ya kisasa ni: “Sikujua”, “Tutabakia wawili” na “Jiwe si mchi”
Baadhi ya mashairi ya kimapokeo ni: “Mahaba”, “mcheza hawi kiwete” “Sivui maji mafu” na mengine.
MATUMIZI YA LUGHA
Vipengele vya matumizi ya lugha vinajadiliwa.
Tamathali za semi
Tashibiha
“Linanuka kama ng’onda” – “Kansa”
Sitiari
“Usijigeuze Popo” – “Itoe kauli yako” “Uchoyo ni sumu” – “Pendo tamu”
Tashihisi
“Inaumwa Afrika” – “Tiba isotibu” “Radi yenye chereko” – “Afrika” “Pendo lenye tabasamu” – “Pendo tamu”
Mubaalagha
“Pendo tamu kama letu duniani hulikuti” – “Pendo tamu”.
Mbinu nyingine za kisanaa
Takriri
Mfano “nilikesha”- “nilikesha” 
“Buzi” – “Buzi lisilochunika”
Matumizi ya semi
Misemo
“mcheza hawi kiwete, ngoma yataka matao” – “Mcheza hawi kiwete”
UJENZI WA TASWIRA
  • Vinyonga” – “viongozi wasaliti mwenye tabia ya kigeugeu” Katika shairi la VINYONGA
  • Miamba”- watu wenye mamlaka/ watu wa tabaka la juu au wale wenye dhamana” katika shairi la MIAMBA
  • Asali"- mwandishi ametumia taswira ya asali akiashiria uhuru uliopatikana toka kwa wakoloni. Katika shairi la ASALI LIPOTOJA 
  • Bundi” – wakoloni wanyonyaji” Katika shairi la BUNDI
  • Jiko –mwanamke asiyejitunza na kujieheshimu yaani Malaya katika shairi la "WEWE JIKO LA SHAMBA"
  • Fahali la dunia”. “Fahali la dunia” – “nchi za ulaya”
  • Wasakatonge –watu wa tabaka la chini (masikini). Katika shairi la WASAKATONGE
  • Tonge la ugali- malighafi katika shaili la TONGE LA UGALI


UHAKIKI WA DIWANI YA MALENGA WAPYA

DIWANI : MALENGA WAPYA WAANDISHI: TAKILUKI
 WACHAPISHAJI: O.U.P
  MWAKA: 1997 
UTANGULIZI
MALENGA WAPYA Ni diwani yenye mkusanyiko WA mashairi yapatayo thelathini na saba (37) yaliyoandikwa na washairi wapya (malenga wapya). Washairi hawa ni wanafunzi wa Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni huko Zanzibar. Katika diwani hii, washairi wamejadili masuala mbalimbali yanayotokea katika jamii. Baadhi yake ni masuala ya kisiasa, kiuchumi, kijamii n.k.Washairi hawa wamejadili masuala ya msingi katika kujenga jamii mpya na kama yatazingatiwa mabadiliko chanya yatatokea kwenye jamii.
MAUDHUI YA MALENGA WAPYA:
 Maudhui ni mawazo yanayozungumzwa na msanii wa kazi ya kifasihi pamoja mtazamo wa mwandishi au msanii juu ya mawazo hayo. 

A). DHAMIRA:
 Ni wazo kuu lililomo katika kazi ya kisanaa.Huu ni msukumo alionao mwandishi hata akaandika kazi Fulani ya kifasihi.Mshairi anaweza kuwa na lengo la kuonesha mambo mbali mbali- mienendo mizuri na mibaya- yatokeayo katika jamii.Katika diwani hii washairi hawa wameyachora mambo kadhaa yatendwayo na jamii, nayo ni kama;

 UONGOZI MBAYA 
Washairi wa diwani hii wamezungumzia suala la uongozi mbaya kama ndicho chanzo cha kudorora kwa maendeleo ya jamii katika Nyanja mbalimbali.Mwandishi ameonesha kuwa viongozi wengi hawatekelezi wajibu wao na pia hawapati muda wa kusikiliza shida za wananchi,viongozi hupuuza kuchukua hatua hata kwa mambo yanayotaka ufumbuzi wa haraka.Kama shairi la PUUZO msanii anasema; 
 Unapokuwa na shida, wao wanakupuuza, Wanajitia kidata, na kuifanya ajiza, Wajifanya hawajali. Ofisini ukifika, wanakuweka baoni, Wakati uliofika,
 wao hawauthamini, Wanakuambia subiri. Hali kadhalika viongozi wengi wadhulumaji kwani huwalazimisha wananchi wanunue hata huduma ambazo kimsingi ni stahiki yao.Katika shairi la BAHARI. Msanii ameonesha dhahiri namna viongozi wanavyotumia nafasi zao kuwakandamiza wananchi.Mshairi anasema 
 Mdai ni haki yao, mola amewajalia Kuwadhulumu wenzao, wao wanafurahia, Nao kwa unyonge wao,wadogo wateketea, Bahari ni hatari,wala usichezee, 
 Katika shairi la MPAKA LINI? Mshairi anelezea kuwa viongozi wana kawaida ya kuwanyanyasa wananchi wanaosema ukweli na kuwakumbatia wale wanafiki na wafitini,kama ubeti huu usemavyo Msema kweli, kwenu nyinyi ni chagizo, Mtaka hali, havuki mbele ya vikwazo, Mwongo Sana, kwenu nyinyi ni kigezo, Mpaka lini mtatuchezea? Pia mwandishi amebainisha jinsi viongozi wasivyo tekeleza ahadi zao na kubaki wanapayuka (kuhutubia majukwaani) mfano katika shairi la PAYUKA (uk 50). Kupayuka kwenu huko, Mbona tu kokoriko, Sioni linalokuwa

MATABAKA
 Mwandishi ameonesha katika jamii kuna matabaka mawili tabaka la chini (tabaka tawaliwa) na tabaka tawala linavyogandamiza na kulinyonya tabalka la chini ( linavyotumikiswa na kulinganishwa na punda) mfano katika shairi la PUNDA msanii anasema;
 “Toka tulipozaliwa, maishayo ni kigozo,kizogo, 
Hatujapata kuenziwa, waishi tingivyogo, Nawe hujajielewa, u kiumbe u kigogo, Kama ungefadhiliwa, usingebeba mzigo, Hakika ulionewa, hustahili kupigwa kipigo, Haki umeitambua, idadi japo kidogo”
Vile vile suala la matabaka limejadiliwa na mwandishi mfano mshairi wa SAMAKI MTUNGONI (UK 19) shairi hili linaonyesha tabaka la juu yaani tabaka tawala (viongozi) ambao ni wavuvi na tabaka la chini yaani tabaka tawaliwa ni samaki, tabaka hili linanyonywa na kugandamizwa. Katika Shairi la NINI WANANGU (UK 24) msanii ameonesha maisha ya chini ya tabaka la chini. Tabaka hli lina hali mbaya ya maisha ukilinganisha na tabaka la juu.

 ATHARI ZA UKOLONI MAMBOLEO 
Ukoloni mamboleo ni hali ya nchi moja kutawala nchi nyingine kiuchumi.Ukoloni mamboleo unaathiri uchumi wanchi zinazoendelea. Katika Shairi NIPATIENI DAWA, mwandishi anaonesha kuwa baada ya ukoloni kuondoka nchini ukoloni huo ulirudi kwa umbo (sura) nyingine ukiendeleza taratibu za kikoloni za kunyonya uchumi wanchi masikini . “Palepale penye donda, ndipo apajanibana, Nikawa sasa nakonda, pumzi nikawa sina, Nikabaki kama ng’onda, la kufanya sikuona, Nipatieni dawa, nipate kutononoka, Kila nikifurukuta, donde apata toa, Najitia kwenye tata, shida kujizidishia, Dawa nimeshatafuta, ili niptate kuoa, Nipatieni dawa, nipate kutononoka.” Mwandishi anaonesha jinsi ukoloni mamboleo ulivozifanya nchi masikini na kunyonya uchumi wake hivyo basi ili kuondokana nao ni lazima atafute dawa. 

NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII Mshairi wa diwani hii amemjadili au amemchora mwanamke katika sura au nafasi tofautitofauti kama ifuatavyo:- A.Mwanamke ni msaliti Katika shairi la UTANIKUMBUKA mwanamke anaonekana ni mtu asiye mwaminifu katika mapenzi na ndoa yake kwa sababu anashiriki ngono na wanaume wenye pesa na mali nyingi huku akimuacha mume wake ambayeni msikini. Mshairi anasema
  “Umeona bora kitu, ukasahau ya nyuma, Umetupa mbali utu, na zote zangu huruma, Kwako kutokaa katu, iko siku utakwama, Utaumeza uwatu, iwe ni yako hatima”. B.Mwanamke ni mtu mwenye tamaa mbaya Katika shairi la UTANIKUMBUKA,mwanamke anaonekana ni mtu mwenye tamaa ya kutaka vitu kutoka kwa wanaume sio kuangalia penzi la mtu. Mwanamke anaonekana kuwa ni mlafi wa mali na mwenye kutamani mali. Mwanamke kama chombo cha starehe(muhuni/Malaya) Katiaka shairi la “KITENDAWILI” mwanamke anaonekana ni chombo cha starehe (mtu Malaya) yaani mtu asiyetulia kwa mwanamme wake (ndoa yake) huku akishiriki mapenzi na wanaume wengine kiasi cha kuogopwa na wengi kwa matendo yake. Mshairi anasema “Jogoo lina mafamba, linatamba kiamboni, Kwa kiburi lajigamba, hadi kiambo jirani, Hili jogoo la shamba, sasa lawika mjini, Kitendawili natega, mteguzi ategue”. Aidha katika shairi la KUUNGE, mwanamke amechorwa kama chombo cha starehe (mtu Malaya) yaani anashiriki tendo la ngono na wanaume wengi ili kukidhi haja ya matamananio ya wanaume. Umalaya husababisha mwanamke kupata magonjwa mbalimbali ikiwemo UKIMWI na hivyo kuwaambukiza wanaume wengi. Mshairi anasema 
“Nawambia silipandi, hii pingu naiweka, Naogopa sina kundi, nikifa la kunizika, Nawapenda kina bundi, na kila anayeruka, Silipandi kataani”. 
Mwanamke ni mtu mwenye mapenzi ya kweli Katika shairi la “NIPATE WAPI MWINGINE” mwanamke anaonekana ni mtu mwaminifu katika mapenzi, mtiifu, na mtu mwenye tabia njema. Ndio maana baada ya kufa,mume wake (mshairi) alimlilia sana. Mshairi anasema: “Njiwa ali maridadi, kwa tabia hana shaka, Na hakuwa mkaidi, umwitapo kakufika, Mafanowe Kama radi, chini inapoanguka, Njiwa ameshanitoka, nipate wapi mwingine”. Mwanamke ni kiumbe dhaifu/duni Katika shairi la “KIFUNGO”, mwanamke anaonekana ni kiumbe dhaifu kisichoweza kufanya chochote cha maendeleo kwani humtegemea mumewe kwa kila kitu na kunyimwa haki yake ya msingi ya kutafuta riziki.Mwanamke hufungiwa ndani ya nyumba pasipo kutoka nje akifanya kazi ya kupika na kulea watoto tu. Mshairi anasema “Kwa kuwa ni mwanamke, ndani munanifutika, Lazima nje nitoke, kupata ninayotaka, Nimechoshwa na upweke, sitaki kudhalilika, Kifungo kimenichosha, minyororo nafungua”.
 UMUHIMU WA KUINUA UCHUMI 
Ili Kujenga taifa linalojitegemea ni lazima kujenga uchumi unaoweza kuleta maendeleo.Mwandishi anaonyesha umuhimu wa kilimo ili kuepukana na adui njaa. Katika Shairi la ADUI msanii anasema; “Tulime jama tulime, tushinde adui njaa, Hapa kwetu ituhame, kwengine kutokomea, Wala sisi tusikome, chakula kujilimia, Tutie jembe mpini, tuteremke shambani, Chakula kujilimia, ziada kujipatia, Tuache kutegemea, vya nje kuagizia, Siku watajigomea, nani tutamlilia? Tutie jembe mpini, tuteremke shambani”. Kwa upande wa kilimo mwandishi ameonesha kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa taifa letu,katika shairi la MKULIMA mwandishi ameonesha kuwa mkulima ni mtu wa kumthamini kwani yeye ndiyo kila kitu kama beti hizi mbili zinazothibitisha; “Wakaazi wa mjini, na wafanya kazi pia, Na viongozi nchini, huduma awapatia, Sijui kakosa nini?, thamani kutomtia, Mkulima naye mtu, yafaa kuthaminiwa” “Upungufu wa chakula, utokeapo nchini, Hukumbana na suala, shambani wafanya nini?, Kazi yako unalala, watia njaa nchini, Mkulima naye mtu, yafaa kuthaminiwa”. Mwandishi anaonesha kuwa jamii inapaswa kumdhamini mkulima kwani anamchango mkubwa katika maendeleo ya taifa. 

UMUHIMU WA KUTENDA MEMA 
Ili jamii iishi kwa utulivu na amani,watu wote hawana budi kutenda mema.Katika shairi la USIHARAKIE MAISHA,waandishi wanataka wanafunzi wanaosoma wasiharakie maisha kwa kutamani vitu vya kesho wakati wao wanaishi leo. Pia katika Shairi la MAISHA NI KAMA NJIA mwandishi anataka jamii itende mema bila kuwatendea wengine uovu hivyo kiburi na ubabe haufai katika jamii (maisha). Pia katika Shairi la ULIMI mwandishi amezitaka ndimi ziseme mambo mazuri tu kama ubeti ufuatao unavyosema; “Usiropoke kwa wenzio, kwanza sema, Usipachike pachike, maneno yasiyo mema, Useme wanufaike kwa kauli yako njema, Ewe ulimi sikia” Mwandishi anaitaka jamii itende mema nyakati zote ili jamii nzima iishi vyema. 
 UMUHIMU WA KUTUMIA PESA VIZURI Mali bila daftari hupotea bila habari. Hivyo amini inaaswa uwe na matumizi mazuri ya pesa, mfano shairi la ISRAFU,msanii anasema; “Mali uliyojichumia, Ni yako nakubalia, Lakini kiangalia, Vipi unaitumia’ Mwenzangu nakuusia, Israfu haifai”. Hivyo matumizi mabaya ya pesa husababisha umasikini ambao husababisha mhusika kukimbiwa na watu hata rafiki zake. 

MAPENZI NA NDOA 
Mapenzi na ndoa ni kitu cha muhimu katika jamii.Mfano shairi laUA mwandishi anasema mtu afikapo umri wa kuoa au kuolewa basi na afanye hivyo shairi la NIPATE WAPI MWINGINE, wasani wanauliza walimwengu wapate wapi wenzi wao baada ya yule wa kwanza kuwatoka.Vilevile wanasema mapenzi ya siku hizi hayafai kwani hutegemea zaidi fedha.Ni mapenzi yenye kusababisha umalaya, yamejaa udanganyifu kati ya mwanamke ana mwanaume mfano shairi la KWA NINI?. Wasanii wanakemea tabia ya baadhi ya wanaume wanaowaacha wake zao na kufanya uzinzi na wanawake wengine wa na kupoteza pesa zao. “Mke wake, atamwacha, singizini, Atoroke, parakacha, migombani, Kumbe kake, anakocha, mwa jirani, Kwa nini?”. Mwandishi anaitaka jamii kuwa na mapenzi ya dhati ili kuepusha maumivu kwa anayeachwa na jamii kwa ujumla. 

UJUMBE 
Waandishi wa diwani hii ya MALENGA WAPYA wanatoa ujumbe ufuatao;
  1.  Kuinua uchumi ni jambo la muhimu sana kwani kutapunguza utegemezi wa misaada kutoka nchi zilizoendelea.Ujmbe huu unapatikana katika shairi la “MKULIMA”, “PUUZO”, “ADUI” na ‘TUYAZINGATIE HAYA”.
  2. Ukombozi wa mwanamke ni muhimu kwaajili yake na jamii nzima. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “KIFUNGO”,“HINA INAPAPATUKA”, na “PUNDA”.
  3.  Hamadi kibindoni silaha iliyo mkononi.Hii ina maana kwamba ni vema kujiwekea akiba kwa kuzingatia matumizi mazuri ya mali, ikiwemo pesa, kwaajili ya maisha mazuri ya kesho. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “ISRAFU”. 
  4. Ili kuinua uchumi wa nchi ni lazima kusisitiza kilimo na kumthamini mkulima. Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “MKULIMA”.
  5.  Jamii izingatie maadili mema ili kuleta haki, usawa na amani. Ujumbe uu unapatikana katika shairi la “HAKI” na “SIHARAKIE MAISHA”.
  6.  Matabaka ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya jamii.Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “SAMAKI MTUNGONI’, “MKULIMA”. 
  7. Maisha ni kama njia.Hapa duniani si makazi ya kudumu,isipokuwa mbinguni.Hivyo tutende mema na tumwombe Mungu ili tuje kuishi maisha ya raha baada ya kifo.Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “MAISHA NI KAMA NJIA”. 
  8. Uongozi mbaya hurudisha nyuma maendeleo ya jamii.Ujumbe huu unapaikana katika shairi la “PUUZO” na “BAHARI”. 
  9. Subira yavuta heri hivyo kila avumiliaye ipo siku atapata.Ujumbe huu unapatikana katika shairi la “SIHARAKIE MAISHA”


FALSAFA 
Mwandishi wa diwani hii anaamini kuwa umoja, amani, na utulivu vitakuwepo endapo haki na usawa miongoni mwa wanajamii vitazingatiwa.Vile vile anaamini kuwa jamii ikitilia mkazo suala la kilimo uchumi wan chi utaimarika sana. 

MSIMAMO/ MTAZAMO
 Waandishi wanamtazamo wa kimapinduzi kwani wamejadili kwa kina matatizo yanayozikabili jamii kama vile matabaka,uongozi mbaya,unyonyaji,ukoloni mamboleo n.k na amependekeza suluhisho la matatizo hayo. 

FANI
 Fani ni umbo la nje ya kazi za fasihi.Katika ushairi vipengele vya fani vinavyochunguzwa ni:- MUUNDO: Hii ni sura, msuko,umbo au uwiano wa vipengele vyote vinavyojenga ushairi. Kuna vipengele kadhaa vinavyotumika kama sehemu ya muundo navyo ni; 
 Tathlitha
Huu ni ushairi wenye mishororo mitatu kwa kila ubeti.Ushairi huu pia huitwa UTATU.Katika kazi hii ya MALENGA WAPYA yapo mashairi kadhaa yaliyosukwa namna hii, nayo ni kama vile PAYUKA, TUNZO, KUUNGE, UA na HALI HALISI. PAYUKA Nasikia makelele, Ya ngoma ile ya lele, Kuimba na kupayuka. 
 Tarbia 
Ni ushairi uliosukwa kwa mishororo minne kwa kila ubeti.Tarbia pia hufahamika kama UNNE.Kidesturi shairi la huwa na mishororo iliyogawanyika katika vipande viwili. Malenga wapya nao wameweza kuisuka kazi yao kwa kutumia muundo huu, mashairi yanayodhihirisha hilo ni pamoja na MAISHA NI KAMA NJIA, ULIMI, SISUMBUKIE KICHAA, NIPATIENI DAWA, NIPATE WAPI MWINGINE na SAMAKI MTONGONI. ULIMI Ulimi ninakuasa, nisemayo usikie, Mwenzio sijenitosa, nafasi sijutie, Ninachokuomba hasa, unifanye nivutie, Ewe ulimi sikia! 
 Takhmisa: 
Ni ushairi wenye mishororo mitano katika kila ubeti.Ushairi huu huitwa pia UTANO au takhmisa. Kuna baadhi ya takhimisa hazina mgawo wa vipande viwili kama ilivyozoeleweka.Katika kazi hii malenga hawa wametumia muundo huu pia kama inavyojidhihirisha katika shairi la ISRAFU, SIHARAKIE MAISHA. ISRAFU Ali ulojichumia, Ni yako nakubalia, Lakini kiangalia, Vipi unaitumia, Mwenzangu nakuusia, israfu haifai. 
 Tasdisa: 
Ni utungo wenye mishororo sita katika kila ubeti. Pia huitwa USITA, TARDISA au TASHLITA. Ingawa tungo hizi si maarufu sana lakini inaonekana katika diwani hii kama inavyojidhihirisha katika shairi la PUNDA msanii anasema; 
Toka ulipozaliwa, maishayo ni kizogo, Hujapata kuenziwa, waishi tirigivyogo, Nawe hujajielewa, u kiumbe hu kigogo, Kama ungefadhiliwa, usingebeba mizigo, Hakika ulionewa, hustahili kipigo, Haki umeitambua, idadi japo japo kidogo.
 Sabilia: 
Ni muundo ambao kazi ya kishairi hujengwa kwa mishororo saba au zaidi kwa ubeti. Kama ilivyo kwa tasdisa mashairi ya namna hii ni machache sana.Katika kazi ya MALENGA WAPYA kuna mfano wa shairi la muundo huu ambalo ni PASUA UWAPE UKWELI.Katika shairi hili msanii anasema; Ambaye tumekuridhi, asili yetu ni moja, Sukani tumekukabidhi, toka zama za mababu, Cheleza lete jahazi, uwapashe wapashike, Pasi kuwa na woga, viduhushi wachochezi, Uyakabili mawimbi, midomo yao wafyate, Na hizo zake tufani, virago vyao wafunge, Zipoze bila muhali, wawafate bwana zao, Kwa kupasua ukweli, visiwa vishuwarike, Kutugawa kwa mafungu, neema iengezeke, Hilo kwetu ni muhali, tufurahie maisha, Si dini wala si rangi, au la hata kabila. 
MATUMIZI YA LUGHA
Katika ushairi kipengele cha lugha huhisisha taswira, tamathali za semi, methali, nahau,misemo na mkato wa maneno. 
Taswira (picha/jazanda)
hiki ni kipengele cha lugha ambacho huchora au huwasilisha wazo kwa kutumia picha au taswira mbalimbali,
mfano katika shairi la SAMAKI MTUNGONI kuna taswira ya samaki ikiwakilisha watu wa tabaka la chini (watawaliwa),
 taswira ya mvuvi ni watu wa tabaka la juu (viongozi) na taswira ya mtungo ni sheria,kanuni au taratibu zinazotumiwa kuwabana watu wa tabaka la chini.
Njiwa mpenzi shairi la NIPATE WAPI MWINGINE? 
Punda- tabaka linalokandamizwa (shairi la PUNDA)
 Ua – mwanamke/ msichana (shairi la UA) 

METHALI
 Kuna methali mbalimbali zimetumiwa katika diwani hii; 
mfano Subira yavuta heri (shairi la SIHARAKIE MAISHA)
 Aisifie mvua kaloa mwilini mwake (shairi la SISUMBUKIE KICHAA) 
Fahari – wapiganapo nyasi ndizo huonewa (SOKOMOKO BAHARINI) MISEMO 
Siharakie maisha (SIHARIKIE MAISHA) Sisumbukie kichaa (SISUMBUKIE KICHAA) Sokomoko baharini (SOKOMOKO 

BAHARINI) TAMATHALI ZA SEMI
 TASHIBIHA 
Ubaguzi umezama kama nguzo (shairi la TUNZO) 
Maisha ni kama njia (shairi la MAISHA NI KAMA NJIA) Yametolewa na kombe mithili ya gome la mti (shairi la BAHAULIM


 TASHIHISI 
Samaki wakasirika (shairi la SAMAKI MTUNGONI) 
Njaa imetuvamia (shairi la ADUI) 
 Ua limejituliza (shairi la UA) 
Ulimi ninakuasa (shairi la ULIM) TASHITITI Katika shairi la MWABAJA MWASEMA NINI? Nasikia mwatunga,mwatungani washairi
 TANAKALI SAUTI 
Parakacha mlio wa majani makvu (shairi la KWA NINI?)
Kokoriko – shairi la MKULIMA
TAKRIRI 
Kuna takriri kituo cha mfano shairi la KWA NINI?
MKATO WA MANENO
Kuna maneno yamekatwa ili kuepuka urari wa vina na mizani mfano “anong’ona (shairi la KWA NINI?).

Monday, April 13, 2020

UHAKIKI WA RIWAYA YA TAKADINI

8UHAKIKI WA RIWAYA RIWAYA YA TAKADINI MWANDISHI: BEN HANSON MCHAPISHAJI: Mathews Bookstore
UTANGULIZI
TAKADINI ni riwaya inayoeleza maisha ya jamii za kiafrika na tamaduni zake.Riwaya hii inaeleza namna jamii nyingi za kiafrika zinavyowakandamiza na kuwanyanyasa watu wenye ulemavu kutokana na mila potofu.Katika riwaya hii mwandishi amemtumia kijana Takadini aliyezaliwa sope alivyowakilisha waathirika wa mila hizo potofu.
 MAUDHUI DHAMIRA KUU; UKOMBOZI
Mwandishi ameeleza kuwa ili tuweze kupata ukombozi wa kweli na kujenga jamii mpya tunapaswa kuachana na mila potofu na kukomboka kifikra na kiutamaduni.Miongoni mwa mila hizo ni mauaji kwa watu wenye ulemavu.Takadini alizaliwa sope aliamriwa auawe siku ya pili tu toka atoke tumboni mwa mamaye Sekai. Aidha makwati anasikitika baada ya kuletewa taarifa kuwa mtoto aliyezaliwa ni sope anasema…..hilositalielewa……itakuwaje….aliuliza maswali mengi (uk 12).Bila ngozi?,Sope?ni nini ulichokileta hapa kwetu?maswali haya yanaonyesha namna walemavu wasivyothamini
wa.Suala hili lilimsononesha sana Sekai inaonyesha dhahiri mtoto sope katika jamii ya Makwati hakustahili kuishi.
 DHAMIRA NDOGO NDOGO MAPENZI Mwandishi anaonyesha mapenzi katika sura mbili tofauti yale ya dhati na ya uongo.Mapenzi ya dhati hayachagui hali wala mali pia kabila dini wala rangi.Kila mtu ana haki ya kupendwa na kupenda Mapenzi ya dhati kati ya Sekai na mwanae, Sekai alikuwa radhi auawe ilimradi furaha yake itimie ya kubaki na mwanawe sope, hakuogopa kufa alimlinda takadini na kuamua atoroke baada ya makwati kuruhusu wazee wamwangamize Mapenzi ya dhati kati ya Sekai na Tendai hawa ni marafiki wa kweli walifarijiana baada ya kuelezana matatizo yao,Tendai mke mdogo wa mtemi masasa aliyelazimishwa kuolewa na mzee wa rika la baba yake. Mapenzi ya dhati kati yaMzee Chivero na Sekai, mzee Chivero alimpokea Sekai na mwanawe Takadini na kuwachukulia kama wanawe (familia yake)licha ya wanakijiji wengine kuwatenga Mapenzi ya dhati baina ya Takadini na Shingai ,Shingai alimpenda Takadini licha ya kuwa na ulemavu wa ngozi (sope)pia mlemavu wa mguu (alitembea kwa msaada wa gongo)kama anavyokiri mwenyewe “huyu ndiye mwanaume ninayetaka anioe” Mapenzi ya uongo ni baina ya Makwati na Takadini, Nhamo na Shangai, Sekai na wake w
enza isipokuwa Pindai
NDOA ZA MITARA
 Mwandishi ameeleza athari za ndoa za mitara kuwa ni pamoja na chuki baina ya wanawake na hivyo kusababisha migogoro ndani ya familia.Mfano Sekai anasengenywa na wake wenza wake Dedirai,na Rumbidzai na kudai ni mchawi. Aidha wake wa Mtemi Masasa wanamdharau Tendai na kuchukulia kama mtoto wao na si mke mwenzao kwa sababu ya umri wake mdogo
 MILA POTOFU
Dhamira hii imetazamwa katika sura tofauti kama vile:- Wazazi kuwachagulia watoto wao wenza (wake/waume)Tendai na Shingai wanalazimishwa kuolewa na watu wasiowataka,hii ni mila potofu zilizopitwa na wakati. Pia Mauaji kwa walemavu, mwandishi anaonyesha kuwa watu wenye ulemavu hawakustahili kuishi katika himaya ya akina Makwati na mtemi Masasa na ndiyo maana kuzaliwa na kuishi kwa Takadini kulileta mzozo. NAFASI YA MWANAMKE Jamii nyingi za kiafrika zinamkandamiza mwanamke na kumfanya mtu duni katika Nyanja mbalimbali za maisha,kama ifuatavyo; Mwanamke hana maamuzi yake binafsi,watoto wa kike hawapati haki sawa na watoto wa kiume.mfano Tendai anaonekana kutofurahishwa na tendo la kuolewa na mume mwenye umri mkubwa (mzee Masasa)alisema “ni heshima kuwa mke wa mtemi mwenye nguvu kama Masasa lakini namchukulia kama baba yangu kuliko mumewangu”…….’’(uk 47)hapa inaonyesha mwanamke hana nafasi ya kuongea kama mtu mwingine. Mwanamke amechorwa kama chombo cha starehe,hili linaonyeshwa kwa mzee Makwati na Mtemi Masasa kuwa na wanawake wengi kwa ajili ya kujifurahisha na hili linajitokeza bayana pale(uk 40) aliletwa mtoto kumpa joto mzee angehisi msisimko wowote ule wa mapenzi. Mwanamke anachorwa kama mwanamapinduzi, haya yanajionyesha wazi kwa Sekai na Shingai ni wanawake walioleta mabadiliko katika jamii.mfano Sekai alikuwa wa kwanza kuvunja mila na desturi kwa kukataa Takadini asiuawe na kuamua kutorokea kijiji cha jirani pia alileta mabdiliko akiwa uhamishoni Shingai naye mwanamapinduzi kwani alipingana na suala kuchaguliwa mchumba aliamini kuwa ndoa ya kweli inahusisha watu wawili waliopendana na waliochaguana alisema “ Si kwamba ninamchukia Nhamo ,la hasha isipokuwa sidhani kama nitakuwa furaha ya kuishi naye”(UK 110)mwisho mwandishi anaonyesha Shingai ameolewa na Takadini na wamezaa mtoto asiye sope. UMOJA NA MSHIKAMANO Umoja na mshikamano ni moja kati ya nguzo muhimu katika kuleta mabadiliko na ukombozi wa kiutamaduni,mshikamano mzuri ulionyeshwa na mzee Chivero,Tendai,mtemi Masasa ulisaidia kumlinda Takadini dhidi ya unyanyapaa na hatari ya kupoteza maisha katika mapambano yoyote yenye umoja na nguvu utengano ni udhaifu UJASIRI Mwandishi ameonyesha kuwa Sekai ni mwanamke jasiri aliepambana kufa na kupona kumlinda mwanae Takadini dhidi ya mila na desturi za kikatili hatima yake kuleta ukombozi katika jamii. Shingai naye ni mwanamke aliyepambana na matatizo ya kuchaguliwa mchumba,mila zinazokandamiza wanawake. SUALA LA MALEZI Malezi ya watoto yanapaswa kusimamiwa kwa pamoja yaani baba na mama.Katika kitabu hiki malezi yanaonekana ya upande mmoja mfano Sekai ndio mlezi mkuu wa familia hususani malezi ya Takadini.Shingai naye anapata malezi kwa mama,shangazi na bibi hata anapokata shauri la kutorokea kwa Takadini ,anaulizwa kuwa ndivyo ulivyolelewa?mzee Nhariswa anampiga mkewe na kusema “umefanya nini wewe mwanamke tangu mwanao alivyopeleka maji kwa Sekai umefuatilia kujua anachokifanya …uliona dalili kwanini hukutafuta dawa? UJUMBE Walemavu wana haki sawa ya kuishi kama watu wengine hivyo wathaminiwe. Malezi yanahusisha pande zote mbili yaani baba na mama hivyo kila mmoja awajibike. Wanawake wawe na maamuzi katika jamii hiyo ili wasinyanyaswe Ndoa nibaina ya watu wawili wapendanao hivyo haipaswi kuingiliwa na mtu yoyote Umoja na mshikamano ni jambo muhimu katika ukombozi wa jamii yeyote ile. MTAZAMO WA MWANDISHI Mwandishi ana mtazamo wa kiyakinifu,anaona kuwa matatizo yanayotokana na mila na desturi yanaweza kukataliwa na watu wengine kwa kuchukua hatua za kujikomboa kama alivyofanya Sekai na wenzake. MSIMAMO WA MWANDISHI Mwandishi ana msimamo wa kimapinduzi kwani ameeleza udhaifu wa baadhi ya mila na desturi zinazokandamiza watu hivyo anataka jamii ijikomboe dhidi ya mila desturi hizo. FALSAFA Mwandishi anaamini kuwa binadamu wote ni sawa hata kama kuna tofauti za kimaumbile lakini kila mtu ana haki ya kuishi . MIGOGORO Migogoro imejitokeza sehemu mbalimbali katika riwaya hii ya TAKADINI kama ifuatavyo; Mgogoro kati ya Makwati na Sekai,chanzo cha mgogoro huu ni (mila na imani potofu) baada ya Sekai kuzaa mtoto sope,mtoto huyo alipaswa auawe ,mwandishi anasema suala hili halikuungwa mkono na Sekai,suluhisho sekai aliamua kutoroka kijijini ili kunusuru maisha ya mtoto Takadini. Mgogoro wa Shingai na wazazi wake,Chanzo cha mgogoro huu ni mila potofu wa kuchaguliwa mchumba ambaye ni Nhamo ambapo wazazi walikasirika hata kumtolea maneno mabaya,suluhisho ni Shingai anaamua kutorokea kwa Takadini. Mgogoro kati ya Sekai na wake wenzake,chanzo cha mgogoro huu ni Makwati kuzidisha upendo kwa Sekai hivyo waliamini kuwa Sekai ni mchawi Mgogoro wa nafsi huu unajitokezakwa Tendai ambaye aliozwa kwa mzee Masasa ambaye alikuwa na umri mkubwa Mgogoro wa kijamii,chanzo cha mgogoro ni kuzaliwa mtoto mlemavu(sope)kulizuka mgogoro baina ya wanajamii ,wao walitaka Sekai na mtoto wake wafukuzwe. MUUNDO Mwandishi ametumia muundo wa msago (moja kwa moja).Mwandishi ameanza mwanzo kuonyesha mimba ya Sekai ambayo inazua chuki kwa wake wenza pia anapozaa mtoto wa kiume (sope). Sekai anaamua kutoroka ili kuokoa maisha ya mtoto,anaishi ugenini siku nyingi hata sope anakuwa mkubwa na kupata mke na mwisho kabisa mwandishi anaonyesha Sekai akipanga kurudi kwao. MTINDO Mwandishi anatumia mtindo wa masimulizi vilevile kuna matumizi ya dayalojia (UK 4) Dadirai na Rumbidzai wanajibizana Je na yule mbuzi wako uliepewa na baba mzee Makwati amekupa watoto wangapi? Tangu nimepata ni miaka miwili sasa na tayari ana watoto wawili nabado anatarajia mwingine. Pia mwandishi ametumia nyimbo (UK 2) Mashamba yote yamelimwa mbegu zote zimepandwa zimechipua na kumea,sisi watatu tumepata mavuno yetu.,Mheshimiwa wetu amemiliki mavuno kwa mikono yake halisi kutoka mashamba yetu yote lakini ni kipi alichoambulia kutoka ardhi ile isiyomea kitu?……….. MATUMIZI YA LUGHA Mwandishi ametumia lugha rahisi inayotumika kwa watu wengi,pia ametumia tamathali za semi,nahau,misemo na mbinu nyingi za kisanaa. MISEMO NA NAHAU Misemo na nahau imetumika katika riwaya hii ili kuipamba kazi yake “Habari njema kuchechemea kwa mguu mmoja lakini mbaya kukimbia kama sungura.Msemo huu unamaanisha kwamba habari njema hazienei haraka ila mbaya huenea haraka sana Pia kuna misemo mingi Kama Pokea upewacho Maosha ni matamu Kanga hawezi kutua kwenye bua la mtama Mume ni kiungo kwa mwanamke TAMATHALI ZA SEMI Tashibiha Matumizi ya tashibiha yamejitokeza sehemu mbalimbali Giza jepesi lilibakia ukutani kama mgeni asiyekaribishwa na asiyetaka kuondoka Muda huenda polepole sana mithili ya mwendo wa kakakuona (UK 6) Tashihisi Mwandishi wa riwaya ya Takadini ametumia tashihisi sehemu mbalimbal; kama vile’ Ubongo wake uliathiriwa kwa mawazo yaliofukuza usingizi wake Fikra zilizopingana zilijichomeka katika nafsi yake Mwanga wa jua ungaavu za novemba uliingia ndani na kulifukuza giza totoro. Dhihaka Mwandishi ametumia tamathali iliyoonyesha dharau na yenye lengo la kumweka mtu katika hali duni kupita kiasi lakini kwa mbinu ya mafumbo (uk 2) “Naamini ulichobeba sasa ni mtoto na si dubwasha” Haya maneno yalimlenga Sekai kwakuwa siku zote waliamini hazai Tafsida Mwandishi ametumia tamathali hii kufichaukali wa maneno (uk 83) Akashambulia hata sehemu za siri (UK 17)walifanya tendo la ndoa Takriri Wewe ni sope,sope,sope Najua ,najua (UK 79) Mdokezo Siku moja sijui lini ….lakini hivi (UK 75) Sukuma mara moja tena ….(UK 125) WAHUSIKA Takadini Huyu ndiye mhusika mkuu wa riwaya hii. Ni mtoto wa Sekai. Ni mlemavu wa mguu na ngozi (zeruzeru ). Kijana wa kiume. Ni mchapakazi na anayependa kujituma.Ni mtiifu.Ni jasiri.Ni mwathirika wa mila na desturi mbaya au zilizopitwa na wakati.Anafaa kuigwa na jamii. Sekai Ni mhusika mkuu. Ni mama yake Takadini. Ni mke wa kwanza wa Makwati. Mwana mapinduzi. Mwathirika wa mila na desturi zilizopitwa na wakati. Ni Jasiri. Ni mwenye huruma.Ni mwenye upendo Makwati Mume wa Sekai.Baba wa Takadini. Ni mkali. Anapendana na mke wake, Anashiriki mila za kale Chivero Ni mzee wa makamo. Ni mganga wa kienyeji. Mwenye upendo. Mwenye huruma.. Ni mshauri mkuu wa Mtemi Masasa.Mpenda mabadiliko. Alimpokea Sekai na Takadini Mtemi masasa Mzee wa makamo. Ni Mtemi wa kijiji. Mwenye heshima. Ni mpole na Mwenye huruma.Mwenye wake wanne. Shingai Ni binti wa mzee Nhasriswa.Mke wa takadini.Ni jasiri. Mwanamapinduzi. Ni msichana mwenye msimamo na mapenzi ya kweli na takadini. Mpenda mabadiliko. Ana huruma .Anafaa kuigwa Tendai Mke mdogo wa mzee Masasa. Ni mke mkarimu. Mwanamapinduzi. Ni mpole .Rafiki kipenzi wa Sekai Dadirai Mke wa tatu wa Makwati.Ni mwenye roho mbaya Mpenda majanga .Ana wivu .Ana mawazo potofu MANDHARI Mwandishi ametumia mandhari ya kijijini.Mandhari hii inawakilisha vijiji mbalimbali hapa Tanzania na Bara la Afrika.Kwa ujumla mahala ambapo hakuna elimu kuhusu ulemavu wa ngozi haijaeleweka vema au hakuna kabisa.Pia vijiji ambavyo huduma kama shule hakuna JINA LA KITABU TAKADINI linasanifu yaliyomo kuwa kuna neno TAKADINI lina maana ya sisi tumefanya nini?Swali ambalo wahusika wengi wanajiuliza mfana Sekai na wanawake wasiozaa na hata vijana au watu wenye ulemavu UCHAMBUZI WA RIWAYA WATOTO WA MAMA NTILIE MWANDISHI: EMMANUEL MBOGO WACHAPISHAJI: HEKO PUBLISHERS MWAKA: 2002 WASIFU WA MWANDISHI Emmanuel Mbogo ni Profesa wa drama na fasihi na amehudumu katika vyuo vikuu mbalimbali ikiwemo, Chuo Kikuu cha Kenyatta Kenya na Chuo Kikuu Huria. Mbogo ni mwanafasihi mahiri sana katika Afrika ya Mashariki. MUHTASARI WA RIWAYA Maman’tilie, mama mwenye watoto wawili lakini wote wamefukuzwa shule kwa kukosa ada na sare. Anajitahidi hapa na pale ili apate, lakini wapi? Pesa imegeuka nyoka inateleza kwenye nyasi. Mumewe Mzee Lomolomo hana muda, yeye kila kukuchapo huelekea bunge la walevi kunywa pombe tani yake. Akiwa huko hunywa na kurudi nyumbani akiwa mbwii! Mwisho mwandishi anauliza swali gumu, ‘Nani anajali?’ MAUDHUI Maudhui hujumuisha mawazo na pengine mafunzo mbalimbali yaliyomsukuma mtunzi ama mwandishi wa kazi ya fasihi akaandika kazi yake. DHAMIRA Dhamira ni lile wazo linalomfanya mwandishi wa kazi ya fasihi aandike kazi yake. Katika riwaya hii, dhamira nyingi zimejadiliwa kama: UMASIKINI Dhamira hii imetawala katika riwaya. Asilimia kubwa ya wahusika ni watu wenye maisha ya dhiki na kazi za kijungujiko. Umasikini wao unadhihirishwa na mitaa wanayoishi kama: Manzese, Msufini, Tabata, Kisutu na Temeke. Maeneo haya ndiyo yaitwayo uswahilini leo hii. Zita na Pita wanafukuzwa shule kwa sababu ya kukosa ada na sare (uk 1). Mamant’ilie naye anatumia maji ya mwarobaini kutibu homa yake kwa sababu hana pesa ya kununulia dawa za hospitali. ULEVI Unywaji wa pombe kupitiliza huweza kusababisha madhara makubwa kwa mtumiaji. Mzee Lomolomo ni mlevi mzoefu, kutokana na ulevi wake, anashindwa hata kuwalipia ada wanae ili waendelee na shule. Ni ulevi huohuo unamfanya aishi maisha ya dhiki huku akishindwa kutoa mchango kwa familia yake na taifa linalomtegemea. Mwisho Lomolomo anakufa kwa sababu ya pombe. Mwandishi anasema, “… Lomolomo alikuwa lofa, mtu wa kazi za kijungujiko na vipesa vyake viliishia kwenye pombe…” (uk 7). MALEZI YA WATOTO Watoto wasipopata malezi yanayostahili kutoka kwa wazazi wote wawili huwa ni rahisi kwao kujiingiza katika mambo yasiyofaa. Mwandishi anaonyesha aina tatu za watoto. Kwanza kuna Zita na Pita. Hawa wana wazazi wote wawili lakini baba hajishughulishi na malezi yao. Pia mama naye ametingwa na shughuli nyingi katika genge lake la uuzaji wa chakula. Zita na Pita hawana malezi ya kueleweka. Hali hii inamfanya Pita ajiingize katika biashara ya madawa ya kulevya. Pili, kuna Dan na Musa hawa hawana baba, wanaishi na mama zao tu. Mama zao hawawajali wala kuwakemea kwa chochote kibaya wanachofanya. Dan anajiingiza katika ujambazi na kupoteza maisha. Musa anajiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya na kuishia jela. Tatu kuna Kurwa na Doto. Hawa hawana wazazi kabisa. mwandishi anasema, “… walikuwa chokoraa namba moja, kupigana kulala na njaa, kukamatwa na polisi… yalikuwa sehemu ya maisha yao…” Doto anajiingiza katika ujambazi, huko anauawa na mlinzi Simango. RUSHWA Rushwa imeota mizizi katika jamii. Kila uendako, kila upitako na kila utokako utaambiwa toa rushwa ili upate kitu fulani. Mamant’ilie alishindwa kuyamudu maisha ya mjini kwa sababu ya rushwa aliyokuwa akiwapa askari wa jiji. Kwa kalamu yake isiyoisha wino, Mbogo anaandika, “KSodi na hongo kwa askari wa jiji, ziliikamua faida yake.” (uk 32). MMOMONYOKO WA MAADILI Maadili ya siku hizi si yale ya zamani. Miaka inabadilika na vizazi navyo vinabadilika. Watu ni watu tu lakini hawana utu. Watoto wadogo sasa wanavuta sigara na kutafuna mirungi kama tumuonavyo Dan na Musa. Watu hawana moyo wa kusaidiana tena, wao wanaamini kuwa kila mwenye janga atalila peke yake. Zita anazidiwa na maradhi yaliyosababishwa na kuumwa na mbwa mwenye kichaa. Watu hawakumsaidia, badala yake walivishangilia vioja alivyovifanya. Mwandishi anatuonesha Zenabu akiwaomba msaada na kuwakalipia, “Nisaidieni, mnacheka nini? Wendawazimu wakubwa.” (uk 82). NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII Nafasi ya mwanamke ni jumla ya matendo yote yafanywayo na mwanamke katika jamii yake. Mara nyingi huwa mabaya na yenye mtazamo hasi, lakini mara chache huwa mazuri yenye mtazamo chanya. Mwandishi wa riwaya hii, amemchora na kumjadili mwanamke kwa mawanda mapana kama inavyoelezwa: Mama mlezi na mwangalizi mkuu wa familia. Maman’tilie ndiye aliyejua familia yake ile nini, ifanye nini na iishi vipi. Mumewe mzee Lomolomo hakuwa na mchango wowote. Yeye kila kukuchapo alikwenda kilingeni kufakamia mataputapu na pombe haramu. Mwenye huruma na moyo wa kutoa msaada. Zenabu anawakilisha tabia hii. Alimsaidia Pita alipokuwa na njaa. Ni yeye akishirikiana na Mama sara walimpeleka Zita hospitali. Mwenye mapenzi na kazi. Kurwa anapenda kazi, alifuatana na Maman’tilie kwenda gengeni, huko alimsaidia kuuza chakula. Hata siku moja kurwa hakuchoka kufanya kazi. Aliyenyimwa elimu. Zita ni mwanamke aliyenyimwa elimu. Anafukuzwa shule kwa kukosa ada na sare. Mzembe na asiyejali malezi ya watoto. Mama Musa ni mzembe na hajali malezi ya mwanae. Yeye ameshika themanini zake na Musa kashika hamsini zake. UJUMBE Ujumbe ni funzo litolewalo na kazi ya fasihi. Mafunzo mengi yametolewa katika riwaya hii: Watoto wasifukuzwe shule kwa sababu ya kukosa ada, kwani kufanya hivyo kunawanyima haki yao ya kupata elimu. Majalala ya kuchoma takataka yajengwe mbali na makazi ya watu. Mwandishi anasema, “Mapafu ya wakazi yaliendelea kuteketea kwa moshi siku hadi siku… watu wale walikuwa wanakufa taratibu.” (uk 27). Pombe si suluhisho la matatizo. Mzaha mzaha hutumbua usaha. Zita alikwaruzwa na mbwa mwenye kichaa, lakini wakapuuzia, mwishi ni kifo cha Zita. MIGOGORO Migogoro ni kukosekana kwa maelewano baina ya watu binafsi, jamii, taifa au mataifa. Migogoro iliyojitokeza ni: Migogoro ya wahusika Mwalimu Chikoya na wanafunzi wasiokuwa na ada wala sare za shule. Huu unasababishwa na wanafunzi wasiokuwa na ada wala sare. Suluhisho lake ni wanafunzi hao kufukuzwa shule. Maman’tilie na mzee Lomolomo. Huu unasababishwa na ulevi wa Lomolomo. Suluhisho ni kifo cha mzee Lomolomo. Peter na Doto. Huu unasababishwa na Doto kumfukuza Pita jaani. Suluhisho la mgogoro huu ni Kurwa kumsaidia Peter. Mgogoro wa nafsi, Huu unampata Peter, yeye anamawazo ya kurudi shule lakini hajui ni kipi afanye ili apate pesa za kumrudisha. Migogoro mingine ni: migogoro ya kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na kijamii. FALSAFA Falsafa ni imani ya mwandishi. Emmanuel Mbogo anaamini kuwasaidia watoto kupata elimu yao kutaondoa matatizo yanayozuia ujenzi wa jamii mpya. MTAZAMO/MSIMAMO Mwandishi anamsimamo wa kimapinduzi. Anaamini kuwapatia watoto elimu na kusimamia malezi yao kutaliokoa taifa. UCHAMBUZI WA FANI NA VIPENGELE VYAKE Fani ni ule ufundi wa kisanaa anaoutumia msanii katika kazi yake. Fani ndiyo hutupatia kile kiitwacho maudhui. Katia riwaya hii, fani imechambuliwa Kama ifuatavyo: WAHUSIKA Wahusika ni watu au viumbe waliokusudiwa uwakilisha tabia za watu katika kazi ya fasihi. Wahusika waliopo katika riwaya hii ni: Maman’tilie. Ni mke wa mzee Lomolomo. Ni mchapakazi. Ni mama yao Zita na Peter na anafaa kuigwa na jamii. Lomolomo. Ni mume wa Maman’tilie. Ni mlevi wa pombe haramu. Hawajibiki katika malezi ya watoto wake na hafai kuigwa na jamii. Zita. Mtoto wa Maman’tilie na mzee Lomolomo. Alifukuzwa shule kwa kukosa ada na sare akiwa darasa la sita. Pia, alikwaruzwa na mbwa mwenye kichaa. Mwisho anakufa kwa kupuuzia ule mkwaruzo wa mbwa. Peter. Mtoto wa Mzee Lomolomo na Maman’tilie. Anafukuzwa shule akiwa darasa la tano. Anatafuta ridhiki dampo. Baadaye anajiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya. Chikoya. Ni mwalimu mkuu wa shule ya msingi Makurumla. Anawafukuza wanafunzi wasiokuwa na sare wala ada. Musa. Anafukuzwa shule kwa kukosa ada na sare. Hamheshimu mama yake. Anajiingiza katika biashara ya madawa ya kulevya. Sara. Mwanafunzi wa Makurumla na ni jirani yao Zita. Mama Sara. Mama yake Sara. Alimsaidia Zita alipopatwa na kichaa. Zenabu. Anafanya kazi Kikale Bar. Ana huruma. Anafaa kuigwa. Kurwa. Ni yatima. Anaishi vichochoroni. Anategemea chakula cha dampo. Anasingiziwa kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya. Doto. Ni yatima. Anauawa kwa kujihusisha na ujambazi. Rhemtulah. Ni mfanyabiashara wa kihindi. Simango. Ni mlinzi wa Rhemtulah. Anawaua Doto na Dan. Dani. Ni mtoto ambaye hamjui baba yake. Anauawa kwa kujihusisha na ujambazi. Jane. Aliwalea Doto na Kurwa baada ya kufiwa na mama yao. Naye pia anakufa. Master Baroni. Anawatumia watoto katika biashara yake ya madawa ya kulevya. Si mfano wa kuigwa na jamii. MATUMIZI YA LUGHA Fasihi ni sanaa itoayo maudhui kwa kutumia lugha ya maneno ambayo hutamkwa au kuandiwa. Kipengele cha lugha ni muhimu kwani ndicho kinachotofautisha fasihi na sanaa zingine. Lugha iliyotumika katika riwaya hii ni nyepesi na yenye kueleweka. Mwandishi ametumia vipengele vingi vipatikanavyo katika matumizi ya lugha kama: ucheshi na lugha ya picha, misemo na tamathali za semi. TAMATHALI ZA SEMI Tamathali za semi ni maneno au sentensi ambazo hutumiwa na wasanii wa fasihi ili kutia nguvu katika maana, mtindo na hata sauti katika maandishi ama kusema. Wakati mwingine hutumiwa ili kupamba na kuongeza utamu wa kazi za fasihi. Mwandishi ametumia tamathali nyingi za semi kama: Tanakali sauti (onomatopoeia). Tanakali sauti ni maneno au nomino ziundwazo katika sentensi kutokana na sauti zinazofanana. “Bwee!” “Paah!” (uk. 5) Tashibiha. Katika tamathali hii, watu ama vitu viwili au zaidi hulinganishwa na watu au vitu vingine kwa kutumia maneno, ‘kama’, ‘mithili’… “Masikio yamesimama wima kama anasisitiza kitu.” (uk. 2) “Mdomo wake uliokaa kama bakuli la pombe.” (uk. 10) Tafsida. Hii hutumika kupunguza ukali wa maneno. “Akaenda haja ndogo.” (uk. 2) “Akakitibu kidonda chake kwa maji ya chumvichumvi.” (uk 55) Takriri. tamathali hii, maneno hurudiwarudiwa ili kuonyesha msisitizo. “Yalaa! Yalaa!” (uk 2) “Mjomba! Mjomba!” Mdokezo. Hapa msemaji husema kitu bila kukimalizia kukitaja. “Shikamoo mama…” (uk 6) “Una… una…” (uk 11) Tashihisi. Hapa vitu hupewa sifa alizonazo binadamu. “Maman’tilie alimtupia jicho bintie.” “Mabega yameangalia juu.” (uk 10). Mjalizo. Katika tamathali hii maneno hufuatana pasipo kiunganishi. “Walikaa, wakala, wakanywa maji, wakamshukuru Mungu.” Kejeli. Hii ni tamathali ya semi ambayo maneno yake huwa kinyume na maana yanayotoa. “Naye pita aliitikia salamu hizo za ukarimu kwa kupiga chafya mbili au tatu.” (uk 19). “Lomolomo uso wake uliopendeza kwa chang’aa…” (uk 70). Sitiari. Tamathali hii hulinganisha vitu bila kutumia viunganishi. “Wakatembea mwendo wa farasi.” (uk 86). Ritifaa. Katika tamathali hii, mtu huongea na kitu ambacho husikika kwa fikra tu. “Kumbe wewe na mwanao mna hila kiasi hiki? Mmepatana kuondoka na kusafiri katika dau moja.” (uk 94). Misemo. “Ukienda Tabata utapata.” “Waswahili hawana dogo.” Matumizi ya lugha za kigeni. “Nikukonekti.” (uk 78). Methali. “Kamba hukatikia pembamba.” Ucheshi na lugha ya picha. “Alikunywa funda moja, akajisikilizia kabla ya kulimeza. Alisikia pombe ikisafiri kufuata barabara ya lami hadi tumboni.” (uk 87). MTINDO Mtindo ni ule upekee wa mtunzi wakazi ya fasihi na mtunzi mwingine. Mfano, mwandishi anaweza kutumia, nyimbo, mashairi, nafsi zote, dayolojia, monolojia n.k. mwandishi amefanikisha mtindo wake kwa kutumia, Matumizi ya nyimbo. Mfano katika ukurasa wa 10 Lomolomo aliimba, “Kuleni nae, Hata bangi vuteni nae, Lakini ni bure, Mwenzenu nimezaa naye…” Mwandishi katumia monolojia (masimulizi) na dayolojia (majibishano). Mwandishi katumia nafsi zote tatu. MUUNDO Riwaya hii imetumia muundo wa kurukia. Mwandishi amemuonyesha Lomolomo akiwa katika hali ya ulevi, baadaye anatukumbusha alipokuwa anafanya kazi bandarini. Vilevile anawaonyesha Kurwa na Doto wakiishi peke yao. Lakini baadaye anatukumbusha kipindi walipokuwa wanalelewa na mama yao ambaye hata hivyo alifariki kisha wakalelewa na Jane ambaye naye anafariki. MANDHARI Mandhari ni sehemu ambayo kazi ya fasihi hutendeka. Riwaya hii imetumia mandhari ya jiji la Dar es Salaam na mitaa yake kama, Manzese, Msufini, Tabata, Kisutu, Urafiki na mtaa wa Ajentina. JINA LA KITABU Jina la kitabu, Watoto wa Maman’tilie, linasadifu yaliyomo, kwani ndani ya riwaya hii kuna mhusika mkuu ambaye ndiye Maman’tilie. Riwaya hii inamwonesha mama huyu akijaribu kujinasua yeye na watoto wake katika wimbi la umasikini, lakini wapi? Jitihada zote anazofanya zinagonga mwamba na matatizo yake yanazidi kuongezeka. KUFAULU KIMAUDHUI Mwandishi amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuonyesha shida wazipatazo watoto wa mitaani. Mwandishi amefanikiwa kuonyesha madhara ya umasikini. Mwandishi ameonyesha madhara ya unywaji wa pombe kupita kiasi na ulevi. KUFAULU KIFANI Amekitendea haki kipengele cha mtindo, kwani humo ametumia vipengele vingi kama nyimbo n.k. Kazi yake imeshibishwa kwa tamathali nyingi za semi. Ametumia lugha ya picha inayomwelewesha zaidi msomaji. KUTOFAULU KWA MWANDISHI 1. Kimaudhui. Mtazamo wa mwandishi katika suala la umasikini hauko sawa. Yeye anaamini hata ukifanya kazi kwa bidii kama ni masikini utaendelea kuwa masikini kama tumuonavyo Maman’tilie. 2. Kifani wahusika wa mwandishi hawana uwiano. Wengi wao ni watu masikini. Pia, mandhari yote yaliyotumiwa na mwandishi ni ya mjini. Mwandishi ameutenga upande wa kijijini ambao nao kama ungetazamwa, jamii ingejifunza mengi. MASWALI YA MAZOEZI Maadili mema na maonyo yamejadiliwa na washairi wa diwani. Onesha mjadala huo kwa kutumia diwani mbili. Ni kwa vipi muundo na mtindo wa ushairi hutofautiana na muundo wa riwaya na tamthilya? Tetea jibu lako kwa kuonesha jinsi muundo na mtindo wa ushairi ulivyo. Ujenzi wa taswira katika kazi za kifasihi hutufanya tuhisi au kuona kabisa uhalisia wa mambo ulivyo. Jadili kwa kutumia diwani mbili ulizosoma. Waandishi wa kazi za fasihi ni walimu? Jadili. Mtazamo, msimamo na falsafa ya mwandishi hututhibitishia ukweli wa mawazo yake katika kazi yake. Fafanua. “Fasihi hubeba yote anayoibusha binadamu katika maisha yake ya kila siku”. Jadili kauli hii kwa kutoa mifano. Fafanua tofauti ya Fasihi simulizi na Fasihi andishi katika vipengele vya fani vifuatavyo: (a) Muundo (b) Mtindo (c) Hadhira (d) Kitanzu Fani na maudhui katika Fasihi ni tunda la marakuja na ganda lake. Jadili kauli hiyo kwa uthibitisho kutoka kwa wataalamu mbalimbali. “Mhakiki ni kivuko kati ya msanii na jamii aliyoiandikia”. Jadili hoja hiyo ukithibitisha kwa mifano madhubuti toka katika kazi za Fasihi andishi za Kitanzania. Fasihi simulizi inaweza kuelimisha au kutoelimisha jamii kutegemea na jinsi ilivyotumika. Thibitisha kauli hii kwa kutumia methali na vitendawili mbalimbali. “Msanii wa Fasihi andishi hutumia vipengele mbalimbali vya Fasihi simulizi ili kuipa kazi yake ubora na mvuto kwa wasomaji wake”. Ukitumia vipengele vitano, fafanua hoja hiyo. Jadili jinsi dhima mbalimbali katika hadithi za Fasihi simulizi zinavyoodhihirishwa na wahusika mbalimbali. “Fasihi inashughulikia utu”. Fafanua usemi huu na thibitisha jibu lako kwa mifano mahususi. “Kila mwanafasihi anatetea tabaka lake”. Jadili kauli hii kwa kutumia mifano ya Tanzania. “Mhakiki wa kazi ya Fasihi ni mnyonyaji wa kazi ya msanii asilia”. Jadili hoja hii kwa mifano. Jadili jukumu la Fasihi simulizi kwa jamii ya Tanzania. Fafanua ni jinsi gani fani na maudhui visivyoweza kutenganishwa katika kazi ya Fasihi. Eleza maana na dhima ya mwandishi wa kazi ya Fasihi kwa wananchi wa Tanzania. Fasihi simulizi inaathiriwa kwa kiasi kikubwa na utandawazi. Jadili kauli hii kwa kutoa mifano halisi.

TAMTHILIYA YA NGOSWE PENZI KITOVU CHA UZEMBE

TAMTHILIYA: NGOSWE PENZI KITOVU CHA UZEMBE
MTUNZI: EDWIN SEMZABA
MCHAPISHAJI: THE GENERAL BOOKSELLERS LTD
CHAPA YA 1-1988
UTANGULIZI
Ngoswe-penzi Kitvu cha Uzembe  inaonyesha namna jamii inapaswa kushiriki mipango mbalimbali ikiwepo ya kisiasa kiuchumi na kiutamaduni.Mafanikio ya mipango hiyo inategemea na kujulikana kwa idadi ya watu utayari,uelewa wa watu hao kuhusu mipango husika Tamthiliya hii inaonyesha kazi ya kuhesabu watu ilivyokwama kijijini kwa mzee mitomingi ngengemkeni kutokana na uzembe wa afisa wa kuhesabu sensa Ngoswe.
DHAMIRA
 MAPENZI
Mwandishi Edwin semzaba ameonyesha jinsi mapenzi yalivyo kitovu cha uzembe,wahusika Ngoswe na Mazoea wametumiwa na mwandishi kufafanua dhamira hii Ngoswe baada ya kufika kwa mzee Mitomingi anashindwa kuitawala nafsi yake mara anapomuona Mazoea,Ngoswe aliamua kuanzisha uhusiano wa kimapenzi na Mazoea hali iliyomfanya ashindwe kuimudu kazi yake na mapenzi kwa wakati mmoja.Ngoswe anamtorosha Mazoea kitendo hiki kinamuudhi balozi Mitomingi Ngengemkeni (baba mzazi wa mazoea)na kuamua kuchoma moto karatasi muhimu za serikali.Ngoswe anaonekani ni mzembe kwa kuwa alishindwa kutofautisha kazi na mapenzi kama msomi (afisa wa sensa) alitakiwa ajue umuhimu wa kazi iliyompeleka kijijini.
 ULEVI NA ADHARI ZAKE
Katika tamthiliya ya ngoswe penzi kitovu cha uzembe mwandishi anaonyesha namna ulevi ulivyoleta madhara,mfano kuchelewesha kazi.Wahusika Mitomingi na Ngoswe wanashindwa kukamilisha kazi kwa vile wahusika (wahesabiwa)wapo kwenye Pombe kama maneno haya yanavyothibitisha;
Mitomingi:Haya ni matatizo yote hii shauri ya pombe nadhani yupo kilabuni
Ngoswe: hawezi kwenda kuitwa?
Mitomongi: haitosaidia mkewe tu hana habari ya kuhesabiwa sembuse hao wengine kwa leo haitowezekana Licha ya kuchelewesha kazi ulevi huaribu kazi.Mfano:ngoswe anaunguza karatasi za sensa baada ya kulewa pombe ya mnazi.
ELIMU
Elimu ni chombo cha ukombozi kama itatumiwa vizuri ipaswavyo,mwandishi wa tamthiliya hii amemuonyesha kijana Ngoswe (msanii)alivyoshindwa kutumia elimu yake hususani katika kujua namna ambavyo  maisha ya mjini yanavyotofautiana na maisha ya kijijini,Ngoswe anajikuta akiharibu kazi yake kwa kukosa maarifa. Mwandishi ameonyesha elimu katika familia ya mito mingi haikupewa thamani yoyote ile wananchi wengi hawakuwa na elimu kwa kisingizio cha shule kuwa mbali, ukosefu wa elimu ulichangia ukosekanaji wa huduma muhimu kama vile hospitali ,miundo mbinu na maji ili kupata maendeleo,suala la elimu lazima litiliwe maanani watu wakieleweshwa wataweza kujua wajibu wao :- Mfano:kujali kazi na kuacha ulevi “kutumia vema hospitali badala ya kutegemea mitishamba
 UCHAWI NA USHIRIKINA
Mwandishi wa tamthiliya hii ameonyesha jinsi watu wengi ndani ya jamii walivyo na imani juu ya uchawi,wanajamii hawa wameweka vikwazo kuhusu sensa wakiamini kuwa mtu anayewahesabu wenzake ni mchawi. Mfano:mama anasema mchawi ndiyo huhesabu watoto wa wenzake ili awaroge sasa wewe ni mchawi?hata kama si mchawi siwezi kukubali unihesabu maana sijui nia yako kama ni mbaya au nzuri.Imani hizo ni za kishirikina zinachangia kukwama kwa zoezi la sensa pia maendeleo kwa ujumla kuwachini,watu wakiugua hawapelekwi hospitali badala yake wanapelekwa kwa mganga wa kienyeji wakidhani kuwa amerogwa.
5. NAFASI YA MWANAMKE
Katika tamthiliya hii mwanamke ametazamwa katika mitizamo tofauti kama ifuatavyo;
Mwanamke amechorwa Kama chombo cha starehe, mwandishi amemuonyesha mzee mitomingi kuwa na wake wengi (mitala) bila kuoyesha bayana kazi zao.
Mwanamke amechorwa kama mtu asiye na sauti .mfano: Mazoea na mama yake hawakushirikishwa katikamipango ya kutaka kuolewa mazoea kwa vile walionekana hawana mchango wowote katika maamuzi hayo
Mwanamke amechorwa kama mlezi, katika tamthiliya hii inamchoramwanamke kama mtu mwenye majukumu ya malezi ya watoto, baada ya Mazoea kuwa namahusiano na Ngoswe mzee Mitomingi anamlaumu mama yake Mazoea kuwa hakuona dalili ya mahusiano ya kimapenzi kwa kuwa ni jukumu la mama kumwangalia binti yake.
NDOA NA MALEZI
Mwandishi wa tamthiliya hii ameonyesha suala la ndoa ni sualala hiyari na si kufuata matakwa ya wazazi, Mazoea alichaguliwa mchumba na wazazi wake (baba yake)hali iliyomfanya kutoroka na ngoswe Hali kadhalika katika tamthiliya hii wanaume wengi wana mke zaidi ya mmoja hali hii inapelekea familia kuwa kubwa na kushindwa kuzitunza. Mfano: Mzee Mitomingi ana wake wawili ambao ni mama Mazoea na mama Mainda, wazazi hawa wanatofautiana katika malezi hasa kwa Mazoea hali iliyopelekea kuwa na tabia mbaya.  Kwa upande mwingine ndoa zenye mke zaidi ya mmoja haziwi na upendo ndani ya familia hivyo kuwa kikwazo kwenye malezi.
UVIVU NA ATHARI ZAKE
Wanakijiji wa Ngengemkeni mitomingi wengi ni wavivu muda mwingi wanautumia kwenye ulevi na uvuvi, unawafanya wakose huduma muhimu kama shule, barabara na hospitali huduma hizi zingepatikana kama wananchi wenyewe wanajitolea. Siku zote wavivu wanatafuta visingizio, vifo vingine vinatokea sababu ya uzembe na uvivu kisha sababu hutafutwa. Mfano:wanawake wawili walidai mume wao amerogwa ili hali wenyewe hawakumpeleka hospitali
 MIGOGORO
Ni hali ya kutoelewana baina ya pande mbili zenye mitazamo tofauti Katika tamthilia ya Ngoswe penzi kitovu cha uzembe kuna migogoro mingi ambayo imeweza kujitokeza Kama ilivyoonyeshwa na mwandishi
Mgogoro kati ya Ngoswe na wazazi wa Mazoea
Chanzo cha mgogoro huu umetokana na Ngoswe kumtorosha Mazoea, suluhisho wazazi kumfukuza Ngoswe na Mazoea kuchoma karatasi na kumwadhibu Mazoea.
Mgogoro kati ya Mazoea na wazazi wake
Chanzo cha mgogoro huu ni baada ya Mazoea kutoroka na Ngoswe ili hali Mazoea tayari ana mchumba wake, suluhisho ni mitomingi kumchapa mazoea na kuchoma karatasi za sensa.
Mgogoro kati ya Ngoswe na serikali,
Chanzo cha mgogoro huu ni Ngoswe kuharibu kazi ya sensa na hivyo kusababishia serikali ishindwe kupanga mipango ya maendeleo, suluhisho halijapatikana hadi mwisho.
UJUMBE
Si jambo zuri kuchanganya suala la kazi na starehe au mapenzi,wakati wa kazi uwewa kazi na wakati wa starehe uwe wa starehe
Wavulana wanaovuruga wasichana siku moja watakamatwa na wasichana wenyewe wanapewa tahadhali wasiwe na maamuzi bila kufikilia.
Elimu ni kitu cha muhimu sana katika jamii na jamii isipokuwa na watu walioelimika hawawezi kuwa na maendeleo maana ili tuwe na maendeleo tunatakiwa tutupilie mbali ulevi na uvivu katika jamii yoyote
Uchawi na ushirikina ni kikwazo kikubwa katika maendeleo

FALSAFA
Mwandishi anaamini kuwa ni rahisi jamii kuingia kwenye matatizo kama itachanganya mambo mengi kwa wakati mmoja hivyo ikumbukwe kuwa kila jambo na wakati wake.
MUUNDO
Muundo uliotumika katika tamthiliya ni wamuundo wa moja kwa moja ambapo kazi nzima ipo katika sehemu tano ambazo mwandishi amezipa majina ya kitwasira kulingana na ukubwa wa tatizo linalozungumziwa ,yaani ameonyesha kuingia kwa Ngoswe kijijini mazingira yanayoashiria hali ngumu ya maisha.
MTINDO
Mtindo uliotumika ni wa kidayalojia ambapo wahusika wake wanazungumza kwa kujibizana Pia kuna matumizi ya nafsi zote tatu na nafsi hizo zimetumika katika sehemu mbalimbali.Mfano sehemu ya tano kwa matumizi ya nafsi ya kwanza pale Ngoswe anapoulizwa na serikali kuhusu takwimu akajibu “usemi sinao”
MANDHARI
Kitabu hiki kimejengwa katika mandhari ya kijijini,hii inadhihirishwa na ukosefu wa huduma muhimu kama vile shule hospitali na miundo mbinu. Tabia za wahusika pia zinaonyesha mandhari ya kijijini mfano, ulevi wa pombe za mnazi,watu kutojali elimu,kun’gan’gania mila zilizopitwa na wakati



MATUMIZI YA LUGHA
Mwandishi ametumia lugha nyepesi na yenye kueleweka pia mwandishi ametumia tamathali za semi,misemo na mbinu nyingi za kisanaa.
Tamathali za semi.
Hizi ni semi au kauli zitumiwazo na mwandishi katika kazi ya fasihi ili kuongeza ladha katika kazi husika
Tashibiha
Ni tamathali ilinganishayo vitu viwili au zaidi kwa kutumia viunganishi kama mithili ya, kama, mfano wa kwa Mfano,
Ngoswe anaposhangaa ardhi ya kijijini kwa balozi Mitomingi anasema Udongo mwekundu kama ugoro wa sabiani
Tazama suruali yake kama kengele ya bomani
Nikitoka hapa najitupa kitandani kama gogo
Tafsida Ni tamathali itumiwayo kupunguza ukali wa maneno. Mfano Mainda anasema labda anajisaidia (UK 21)
Takriri ni tamathali inayorudiarudia neno ili kuweka mkazo juu ya kile kinachosemwa Mfano; karibu, karibu (pale Ngoswe alipokuwa akikaribishwa)
Mdokezo Ni tamathali ambayo hueleza jambo kwa kukatakata maelezo Mfano Mazoea anasema sijui……sijui……siwezi namwogopa baba (Uk 22)
Tanakali za sauti Ni tamathali inayoiga mlio wa vitu mfano Ngoswe alishindwa kujizuia akacheka ha ha ha ha
Methali
Ngoswe anamwambia Mazoea v  “Penye nia pana njia” (uk 22)
Misemo
Hebu keti tutupe mawe pangoni
 Kupeleka chakula ndio unafanya makambi
WAHUSIKA
Wahusika ni watu walioshiriki katika mchezo au tamthiliya husika. 
NGOSWE
Ni msomi anayependa kazi ya kuhesabu watu lakini kutokana na tamaa ya mwili wake anaharibu kazi baada ya takwimu zote kuchomwa moto na Mitomingi kutokana na kitendo cha kujaribu kumtorosha mazoea .
Mazoea
Ni Msichana mwenye umri wa miaka 18-20. Ni motto wa balozi (Mitimingi). Anawakilisha   wanawake wasio na msimamo katika mapenzi

Ngengemkeni mitomingi
Huyu ni balozi. Ni  Baba yake Mazoea Anachoma karatasi za takwimu kutokana na Ngoswe kutaka kumtorosha Mazoea. Ni mzee aliyeshikilia ukale na anapenda ndoa za mitara.
JINA LA KITABU
Ngoswe penzi kitovu cha uzembe jina hilo la kitabu linasadifu yaliyomo ndani ya kitabu, kwani msanii kwa kiasi kikubwa amejaribu kujadili na kuonyesha matatizo yanayoikumba jamii katika shughuli za kijamii,matatizo hayo ni kama uchawi ulevi uzembe na dhana nyingine potofu.
KUFAULU NA KUTOFAULU KWA
MWANDISHI
 Mwandishi katika tamthiliya hii amefeli kwa kuwa ameonyesha matatizo yaliyomo katika jamii bila kuonyesha mbinu mbadala ya kuyatatua.

TAMTHILIYA YA KILIO CHETU

UHAKIKI WA TAMTHILIYA
TAMTHILIYA: KILIO CHETU
WAANDISHI: MEDICAL AID FOUNDATION
MCHAPISHAJI: TANZANIA PUBLISHING HOUSE (TPH) MWAKA 1995
UTANGULIZI
Kilio Chetu ni tamthiliya inayojikita kuzungumzia umuhimu wa elimu ya jinsia na ukimwi kwa vijana, Tamthiliya hii inaonesha namna ukosefu wa elimu ya jinsia na ukimwi kwa jamii hususani vijana inavyochangia mimba za utotoni au mimba zisizotarajiwa na maambukizi ya virusi vya ukimwi kwa vijana.
Katika tamthiliya hii, mwandishi anaonesha namna ambavyo jamii ikiangaika kujielimisha kuhusu elimu hii ya jinsia na ukimwa na kuwaacha vijana wakiangamia kwa kukosa elimu hiyo, hali hii inaifanya jamii kugawanyika, wapo wanaoona kuwa suluhisho la janga hili la Ukimwi, ni jamii nzima wakiwemo na vijana kupewa elimu hii lakini wapo wazazi wanaopinga wakiamini vijana umri wao wakupewa elimu hii haujafika bado. Je ni nini hatima ya vijana hawa? Basi tafuta kitabu hiki cha Kilio chetu kisome utajifunza mambo mengi sana ni kitabu kinachotakiwa kusomwa na watu wa rika lolote.
DHAMIRA
Hili ni wazo kuu au mawazo mbalimbali yanayojitokeza katika kazi ya fasihi. Na katika tamthiliya hii kuna dhamira kuu na dhamira ndogondogo ambazo zimejitokeza, kwa kuanza tunaanza na;
(a)  Dhamira Kuu
Dhamira kuu katika tamthiliya ni umuhimu wa elimu ya jinsia na ukimwi, mwandishi anaamini kuwa, ili jamii iweze kunusurika na matatizo yatokanayo na kujamiana kama vile mimba za utotoni (mimba zisizotarajiwa) magonjwa ya zinaa kama vile kasendwe, kisonono gono na ukimwi, sharti vijana wapewe elimu ya jinsia na ukimwi, mwandishi anathibitisha hili akimtumia muhusika Mjomba anaposema, “Upepo umebadilika sasa. Hawa vijana wetu wapewe elimu ya familia ikiwepo ya jinsia. Watoto waambiwe wazi juu ya mambo haya ya mapenzi na hatima yake.” Uk. 9
Vilevile, mwandishi anaonesha namna ambavyo vijana wanapukutika, wanaangamia na ukimwi kwa sababu ya kukosa elimu hii ya jinsia na ukimwi, hali hii inasababisha vijana kuwa gizani kabisa wanashindwa namna ya kujikinga na wengine hata kushindwa kutofautisha kati ya puto na kondomu , rejea ukurasa wa 13, Mwandishi akimtumia muhusika Mtambaji anaposema, “Kisiwa kizima kipo gizani. Watoto ndio kabisa. Wapo katika giza nene. Wanashindwa kutofautisha kati ya puto na kondomu.”
Si hivyo tu, mwandishi anaendelea kutuonesha kuwa, ukosefu wa elimu hii ya jinsia na ukimwi kwa vijana/watoto inawafanya watoto/vijana kujitenga na mapambano dhidi ya ukimwi kwakuwa wao wanaamini kuwa ugonjwa huu wa ukimwi ni wa wakubwa tu kwani watoto hawawezi kuambukizwa virusi vya UKIMWI kama mwandishi anavyosema akimtumia muhusika Mwarami anapomwabia Anna, “Ukimwi unawapata wakubwa, Anna.” Uk. 25
Si watoto tu, wapo hata wazazi, watu wazima ambao nao wanaamini kuwa watoto wadogo hawawezi kuambukizwa virusi vya ukimwi, kama anavyoamini Mama Suzi, rejea ukurasa wa 4, muhusika Mama Suzi anaposema, “…Lakini shoga, watu wanatafuta laana ya marehemu. Kitoto kama kile; kife kwa ukimwi! Ungeingilia kona gani?” {Uk.4}
Mwandishi anaendelea kutuonesha kuwa, hata mimba za utotoni, mimba zisizotarajiwa kwa vijana husababishwa na ukosefu wa elimu hii ya jinsia, kwa mfano mwandishi anamtumia muhusika Suzi ambaye anaamini kuwa, kwa kufanya ngono mara moja hakuwezi kusababisha mtu akapata mimba, hili tunaliona ukurasa wa 28, Suzi anapomwambia Anna, “Wala sina mimba, kwanza mimi nimefanya mara moja tu na joti.” {Uk.28}
Vilevile, mwandishi anaonesha kuwa, wapo watoto/vijana ambao kutokana na kukosa elimu hii ya jinsia, wanaamini kuwa wao kama watoto hawawezi kupata mimba, mwandishi anamtumia muhusika Joti anapowaambia rafiki zake, “Mara moja tu, hakuna mimba sisi watoto.” {Uk. 16}
Mwandishi hakuishia tu kuonesha madhara ya kukosa elimu hii ya jinsia, kwa upande mwingine ameonesha faida za elimu hii ya jinsia na ukimwi kwa vijana, mwandishi anaonesha kuwa, vijana waliopata elimu hii, huwasaidia sana kupambana na kujizuia na vishawishi vya kingono kutokana na uelewa waliokuwa nao, kwa mfano mwandishi anamtumia muhusika Anna, ambaye kutokana na mafunzo aliyopewa na wazazi wake yanamsaidia sana kupambana na kujizuia na vishawishi hivyo kutokana na kufahamu madhara ya kushiriki ngono kabla ya wakati, hili mwandishi analithibitisha akimtumia muhusika Anna anaposema, “…Hujui kama kuna madhara mengine. Hujui magonjwa ya zinaa wewe: hujui kisonono, kaswende na mengine kedekede. Haya hata UKIMWI hujui?”  {Uk. 25}
Hivyo mwandishi anashauri, elimu hii ya jinsia na UKIMWI, isitolewa kiubaguzi, itolewe kwa watu wote kwani kila mtu yuko katika hatari ya kuambukizwa virusi vya UKIMWI, mwandishi anaonesha namna ambavyo vijana wanateketea kwa kubaguliwa kwao kupewa elimu hii, rejea ukurasa wa 1-2, Mtambaji anaposimulia, “Wakubwa wakaandika mabuku kupeana habari. Wakabandika mabango kupeana tahadhari, lakini watoto wakateketea kwa kukosa habari zozote za kuwaokoa.”
Mwandishi anaonesha kuwa, kama vijana wangeelimishwa kuhusu madhara ya kufanya mapenzi kabla ya wakati, namna ya kujilinda, basi wasingetummbukia katika janga hili, mwandishi anathibitisha kwa kumtumia muhusika Suzi anaposema, “Naapa kwa Mungu wangu, mimi na Joti tungepata bahati ya kuelimishwa, tusingetumbu…tusi… (Anaanguka chini.)” {Uk. 36}
(B) DHAMIRA NDOGO NDOGO
1.     Ukosefu wa elimu
Dhamira hii inajitokeza katika tamthiliya, mwandishi anaonesha kuwa ukosefu wa elimu ya namna ya kupambana na Ukimwi unaifanya jamii kushindwa kulikabili gonjwa hili, ukosefu wa elimu unawafanya wengine kuamini ugonjwa huu ni wa kurogwa, wengine wanaamini ni ugonjwa unaletwa na mizimu na hata wengine kudhani ni majini.
2.     Mapenzi na ndoa
Suala la mapenzi na ndoa pia limepewa nafasi katika tamthiliya hii, tukianza na suala la mapenzi, mwandishi anajadili mapenzi ya namna mbili, mapenzi ya dhati na mapenzi ya ulaghai.
(a)  Mapenzi ya dhati
 Baba Anna kwa familia yake. Mjomba kwa Suzi.Anna kwa wazazi wake.Anna kwa Suzi.Suzi kwa Joti
(b) Mapenzi ya ulaghai
Joti kwa Suzi. Joti kwa Chausiku.Chausiku kwa Joti
3.     Malezi kwa vijana
Mwandishi pia amegusia suala la malezi kwa watoto, mwandishi anaonesha kuwa, malezi bora kwa mtoto ni malezi ya wazazi wote wawili, yaani baba na mama, na anapokosekana mzazi mmoja huweza kumuathiri mtoto, katika tamthiliya hii tunamuona Suzi akilelewa na mama peke yake bila baba hali hii inachangia mtoto kuingia katika matatizo, hili linathibitishwa na mwandishi akimtumia muhusika Mama Suzi anaposema, “Kila siku ninasema mwanangu mdogo, mwanangu ni mtoto mzuri, leo Suzi unanifanyia hivi? Hivi baba yako angekuwepo ungefanya hivi? Ah Suzi, ungefanya?” {Uk.31}
Katika suala hili la malezi, mwandishi anatuambia kuwa kuwa, mzazi ndiyo mwalimu bora kwa malezi mema ya mtoto,rejea ukurasa wa 11, Mjomba na Baba ANNA wanaposema, “Mzazi ndiye mwalimu wa kwanza…Na ndiye bora.” {Uk. 11} hivyo wazazi wawafundishe vema watoto wao, lakini wazazi wasipofanya hivyo, walimwengu watawafundisha na kwa kawaida walimwengu hufundisha katika upotofu, rejea ukurasa wa 10-11, Baba Anna anaposema, “Dunia imeharibika bwana. Mzazi usipomfunza, walimwengu watamfundisha tena sasa si maadili mema bali njia potofu.” {Uk.10-11}
4.     USALITI
Usaliti ni dhamira nyingine inayojitokeza katika tamthiliya hii, kwa mfano mwandishi anaonesha usaliti unaofanywa na Baba Joti kwa mke wake, Baba Joti anaisaliti ndoa yake kwa kuanzisha uhusiano wa kimapenzi na mwanamke mwingine, hili linathibitishwa na Mama Anna anaposema, “Lakini leo nimefika kikomo. Ndiyo mwisho wa kumvumilia huyu nguru anayeichimba ndoa yangu.” {Uk. 7}
Usaliti mwingine, tunaona kwa Joti, pamoja na kwamba Joti anakuwa na mahusiano ya kimapenzi na Suzi anaamua kumsaliti na kuanzisha mahusiano na wanawake wengine, mwandishi analithibitisha hili akimtumia muhusika Suzi anaposema, “Ndiyo maana mie nilikuwa nakataa Joti. Nishaambiwa kwamba unawasichana wengi shuleni na mtaani kwetu.” {Uk. 21}
Usaliti mwingine unajitokeza kwa Joti na Chausiku, mwandishi anaonesha kuwa Joti pamoja na kuwa na mahusiano na Chausiku anamsaliti Chausiku kwa kuwa na mahusiano na wasichana wengine, Joti anapewa vitu na Chausiku naye anawapa wanawake wengine, rejea ukurasa wa  22, Chausiku anaposema, “Toka hapa. Nimesikia habari zako. Kila msichana unamtaka tu. Mie nakununulia fulana ya mazoezi wewe unahonga kinyago chako kile. Bisha…Nikikupa hela ya kununua peni we unanunulia bazooka visichana vyako.” {Uk. 22} lakini si Joti tu ndiye anamsaliti mwenzake, mwanandishi anatuonesha kuwa, hata Chausiku pia, anamsaliti Joti kwa kuwa na mahusiano na wanaume wengine, rejea ukurasa wa 22-23, Mwarami anapomwambia Joti, “Sasa ndiyo kuparamia mpaka wasichana wakubwa wa mtaani? Fikiri juu ya Chausiku, Yule msichana mjuvi wa mji ambaye pia anachukuliwa na Yule mpemba muuza duka.” {Uk. 22-23}
5.     ATHARI ZA UTANDAWAZI
Mwandishi pia amejadili suala la utandawazi na athari zake, mwandishi anaonesha namna utandawazi unavyochangia kwa kiasi kikubwa kuharibu tabia na maadili ya watoto na vijana, kwa mfano tunawaona akina Joti, Jumbe, Choggo na Mwarami wanajiingiza katika mahusiano ya kingono wakiwa watoto wadogo kutokana na kuathiriwa na video za ngono (sinema za X) wanazozitazama mtaani, mikanda hii ya ngono imekuwa rahisi sana kupatikana kutokana na utandawazi.
6.     ATHALI ZA UKOLONI NA UKOLONI MAMBO LEO
Suala la ukoloni na ukoloni mambo leo pia limepewa nafasi katika tamthiliya hii, mwandishi anaonesha namna  wakoloni walivyoharibu utamaduni wetu kwa kuuita ushenzi na hata tulivyopata uhuru, viongoni wetu wakaendelea kushikilia mawazo hayo potofu ya kikoloni ambayo kwa kiasi kikubwa tunaangamia wenyewe, hili mwandishi analithibisha akimtumia Mtambaji anaposema, “Mila zetu hazikukataza kutoa mafunzo ya elimu ya jinsia…Wakoloni na vibaraka wao ndio wanaostahili kulaumiwa wakoloni walipiga vita jando na unyago wakidai eti ni ushenzi.” Mtambaji anaendelea kutuambia tena, “Viongozi wetu nao wakaendeleza mawazo hayo hata baada uhuru bila kutambua kuwa wanajiua wenyewe.” {Uk. 13-14}
7.    NAFASI YA MWANAMKE KATIKA JAMII
Mwanamke amechorwa kama mlezi wa familia, mwandishi anatuonesha namna ambavyo mwanamke anakuwa mlezi mzuri wa familia, anaangaika hapa na pale kuhakikisha mtoto au watoto wake wanapata mahitaji yote muhimu kama vile chakula, mavazi na hata elimu, rejea ukurasa 30, Mama Suzi anaposema, “Mimi ninahangaika kukusomesha, wewe unanifanya hivi…Mama yako nimeungua viganja kwa kupika vitumbu ili mwanangu usome.” {Uk. 30}
Mwanamke amechorwa Kama mtu mwenyemsimamo, mwandishi anamtumia muhusika Anna kumuonesha mwanamke kama mtu mwenye msimamo katika maamuzi yake, tunamuona Anna pamoja na kusumbuliwa mara kwa mara na Mwarami kumtaka kimapenzi bado anashikilia msimamo wake ule ule wa kumkatalia, hata watu wazima wenye uwezo kipesa wanapomtaka Anna bado Anna anaonesha kutoyumba kimimamo kwa kuwakatalia. Rejea wimbo anaoimba Anna ukurasa wa 27,
       “Anna Anna Anna mie niacheni mie x2
      Msichana mdogo bado nasoma niacheni mie.
     Muda wangu kufanya hayo haujafika mie.
           Pesa zenu, na lifti zenu niacheni mie.
          Anna Anna Anna mie niacheni x2”
Mwanamke amechorwa kama mtu anayepinga mabadiliko katika jamii, mwandishi anatuonesha kuwa mwanamke ni mtu asiyependa mabadiliko katika jamii, asiyependa kwenda na wakati, dunia inabadilika jamii inatakiwa kuwaelimisha vijana wao kuhusu elimu ya jinsia na mahusiano ,Mama Suzi anapinga, rejea Mama Suzi anaposema, “Tena ishia hapo hapo kaka! Huko si kunifundishia mwanangu umalaya? Umfunze mwanangu habari za ngono ilitoka wapi hiyo? {Uk. 9}
Mwanamke amechorwa kama mtu asiye na msimamo, mwandishi anatuonesha kuwa, mwanamke ni mtu asiye na msimamo katika maamuzi yake, mwandishi anamtumia Suzi, kuijadili nafasi hii, richa ya Suzi kuamua kuachana na Joti na hata anapogundua kuwa Joti anamahusiano na wanawake wengine bado anakubali kuendelea naye. (Rejea uk. 17 na 21)
Vile vile, mwandishi amemchora mwanamke kama chombo cha starehe,Anamtumia mhusika Joti ambaye anawatumia wanawake ili kujistarehesha kingono, lakini pia tunaona namna watu wanavyotumia pesa na vitu vya thamani ili kuwarubuni wasichana wapate kukidhi mahitaji yao ya kingono. {rejea ukurasa 27}
Mwanamke amechorwa kama mtu asiye na elimu juu ya mambo ya jinsia na ukimwi, katika kuilezea nafasi hii, mwandishi anamtumia mhusika Mama Suzi, ambaye anaoneka kutokuwa na ufahamu mzuri juu ya masuala ya UKIMWI, kwa mawazo yake anaamini kuwa ugonjwa wa UKIMWI ni ugonjwa unaowahusu watu wakubwa tu, na watoto hawawezi kuambukizwa jambo ambalo si sahihi. Hata katika jamii yetu, wapo watu wanaoamini kuwa ugonjwa huu wa UKIMWI huwakumba watu wazima watoto na watu walio katika ndoa hawawezi kuambukizwa virusi vya ukimwi jambo ambalo si kweli. Hivyo jamii inatakiwa kuelimishwa sana kuhusu ugonjwa huu.
WAHUSIKA
Katika kazi ya fasihi wahusika wanaweza kuwa watu, wanyama au vitu, na wahusika ndiyo wanaobeba dhamira za msanii, na katika kazi ya fasihi wahusika tunawagawa katika makundi mawili, wahusika wakuu na wahusika wasaidizi/ wahusika wadogowdogo
(a)  Wahusika Wakuu
Katika tamthiliya hii, ina wahusika wakuu wawili, ambao ni Suzi na Joti.
1.     SUZI
Ni binti anayesoma shule ya msingi
Ni binti asiyekuwa na elimu ya jinsia na ukimwi, Mama yake anashindwa kumpa elimu hiyo akiamini kuwa umri wa Suzi haujafikia kupewa elimu hiyo.
 Anajiingiza katika mapenzi akiwa mdogo.
Anakuwa na mahusiano ya kingono na mwanafunzi mwenzake anayeitwa Joti.
 Ni binti wa pekee wa Mama Suzi.
Anapata mimba akiwa mwanafunzi na anafikiria kuiotoa mimba hiyo.
2.     JOTI
Ni kijana wa kiume anayesoma shule ya msingi.
Ni kijana asiyekuwa na elimu ya jinsia na ukimwi, baba yake anashindwa kumpa elimu hiyo akiamini kuwa umri wa joti haujafikia kupewa elimu hiyo.
Anajiingiza katika mahusiano ya kingono akiwa mdogo huku akiwa mwanafunzi.
Anajihusisha na mahusiano ya kingono na wasichana wengi, akiwemo Suzi, Chausiku, Gelda n.k.
Ni mvulana mlaghai, anawalaghai wasichana ili tu kutimiza haja zake za kingono.
Anaambukizwa virusi vya ukimwi
Anafariki kwa ugonjwa wa ukimwi.
(b) Wahusika wadogo wadogo
1.     MAMA SUZI
Huyu ni mama yake Suzi. Anamlea Suzi bila baba. Anajishughulisha na biashara ndogondogo kama vile kuuza vitumbua ili kujipatia kipato. Anaamini kuwa mtoto mdogo hawezi kuambukizwa virusi vya ukimwi. Anakumbatia mila na desturi zililozipitwa na wakati zinazokataza watoto/vijana kupewa elimu ya jinsia na ukimwi.Anakataa katakata mtoto wake, Suzi kupewa elimu ya jinsia na ukimwi akiamini kuwa umri wake ni mdogo, na kufanya hivyo ni sawa na kumfundisha umalaya.Anamwadhibu mtoto wake (Suzi) baada ya kukuta vidonge vya kuzuia mimba katika mfuko wa sketi yake.
2.     BABA JOTI
Ni baba yake na Joti.Anaamini kuwa ukali wa mzazi na viboko ndiyo suluhisho la kuwazuia watoto kujiingiza katika mambo mabaya. Anakataa katakata elimu ya jinsia na ukimwi kutolewa kwa watoto/vijana.Anaangaika kuokoa uhai wa mtoto wake, Joti, kwa kutafuta tiba yake kila mahali. Anampoteza mtoto wake (joti) baada ya kufariki kutokana na ukimwi.
3.     MAMA JOTI
Huyu ni mama yake Joti.Mke wa Baba Joti. Rafiki yake Mama Suzi. Anahisi mume wake ana uhusiano wa kimapenzi na wanawake wengine, hali inayomlazimu kuwanunulia kanga zenye maandishi ya mafumbo ili kuwapasha wezi wake.Yeye na mumu wake (Baba Joti) wanashindwa kumpa Joti elimu ya jinsia na ukimwi.
4.     BABA ANNA
Huyu ni baba yake Anna.Anaamini kuwa elimu ya jinsia na ukimwi ni muhimu kwa vijana ili kuwanusuru na janga la ukimwi.Kwa kushirikiana na mke wake wanafanikiwa kuwapa watoto wao elimu ya jinsia na ukimwi, elimu inayowasaidia kupambana na vishawishi.
5.     MAMA ANNA
Huyu ni mama yake Anna. Ni mke wa Baba Anna.Kwa kushirikiana na mume wake wanafanikiwa kuwapa watoto wao elimu ya jinsia na ukimwi, elimu inayowasaidia kupambana na vishawishi.
6.     ANNA
Mtoto wa kike wa Baba Anna na Mama Anna.Ni mwanafunzi wa Shule ya msingi.Amepewa elimu ya jinsia na ukimwi, elimu inayomsaidia kupambana na vishawishi vya kujiingiza katika mahusiano ya kimapenzi akiwa mdogo.Ana mkatalia Mwarami kuwa naye kimapenzi.
Wahusika wengine katika tamthiliya ya kilio chetu ni jirani, mwarami, chogo, mjomba, jumbe, fausta, chausiku na mpemba.
MIGOGORO
Migogoro ni hali ya kutoelewana baina ya pande mbili, unaweza kuwa mgogoro kati ya mtu na mtu, mtu na kikundi cha watu, kikundi kimoja na kikundi kingine cha watu au unaweza kuwa mgogoro wa mtu na nafsi yake. Katika tamthiliya hii, mwandishi ameweza kuibua na kuonesha migogoro mbalimbali ambayo kwa kiasi kikubwa migogoro hiyo imeweza kusaidia katika ujenzi wa dhamira mbalimbali zilizoweza kujitokeza katika kazi hii, migogoro iliyojitokeza katika tamthiliya hii ni:
Mgogoro kati ya Mama suzi na mwanaye,(Suzi) chanzo cha mgogoro ni Mama Suzi kukuta kasha la vidonge vya kuzuia mimba kwenye mfuko wa sketi ya Suzi, mgogoro unakua zaidi Mama Suzi kuamua kumuadhibu kwa kumchapa Suzi hadi anapotokea Mjomba na Baba Anna, kuamulia mgogoro huo na kushauri jambo la msingi ni kumpa elimu ya jinsia na si kutumia ukali na viboko, kama ambavyo Baba Anna anasema, “Watoto wajazwe elimu, waone uchafu na hatari ya kufanya haya. Siyo kuwatia hofu tu. Je leo ukifa ama kulazimika kuwa mbali nawe? Si atafanya tu maana mtia hofu hayupo?” {Uk. 13}
Mgogoro kati ya Mjomba na Mama Suzi, chanzo cha mgogoro ni kitendo cha Mjomba kumshauri Mama Suzi kuacha kumuadhibu Suzi na badala yake apewe elimu ya jinsia na mahusiano ya kimapenzi jambo linalopingwa na Mama Suzi na hivyo kuibua mgogoro. {Rejea ukurasa wa 8-14}
Mgogoro kati ya Suzi na Joti, mgogoro huu unaibuka baada ya Suzi kupigwa na mama yake sababu ya vidonge vya kuzuia mimba alivyopewa na Joti, mgogoro huu unafikia hatua ya Suzi kuamua kuachana na Joti, suluhisho la mgogoro huu, wanaamua kurudiana na kuendelea na uhusiano wao. (Rejea uk. 17 na 21)
Mgogoro kati ya Mwarami na rafiki zake yaani Jumbe, Joti na Choggo. Chanzo cha mgogoro ni kitendo cha Mwarami kutokuwa na uhusiano wa kimapenzi na wasichana, hatua inayosababisha kumtishia kumfukuza katika kundi lao, rejea ukurasa wa 24, Jumbe anapomwambia Mwarami, “Sasa bwana hapa kwenye grupu letu hatutaki tabia hiyo ya ushamba. La sivyotutakutoa umemba.” Suluhisho la mgogoro huu ni Mwarami kuamua kumshawishi Anna kimapenzi hata hivyo juhudi zake zinagonga mwamba.
Mgogoro kati ya Mama Joti na Mwanamke anayedhani anaingilia ndoa yake,Mama Joti anaona suluhisho la mgogoro huu ni kununua kanga zenye maneno ya vijembe ili kumpasha na kumuumiza roho, Rejea Mama Joti anaposema, “Lakini leo nimefika kikomo. Ndiyo mwisho wa kumvumilia huyu nguru anayeichimba ndoa yangu…Ngoja kwanza nimpashe najua litamuuma tu.” {Uk. 7}
Mgogoro mwingine ni kati ya Chausiku na Joti, chanzo cha mgogoro huu ni baada ya kugundua kuwa Joti anamahusiano ya kimapenzi na wasichana wengine, mgogoro unafikia hatua ya Chausiku kumtishia kumdhuru Joti, kama anavyosema, “We usinifanye mie bwege mwenzio…wewe ndiyo unajigonga gonga. Wewe na visichana vyako hivyo nitawachoma moto mie! Nyie hamnijui, ohoooo!” {Uk. 22}
Mgogoro wa Suzi na nafsi yake, chanzo cha mgogoro huu ni kitendo cha kuambiwa na mama yake kuwa shangazi yake ataenda kumpima mimba, Suzi anaona suluhisho la mgogoro huu ni kutokubali kwenda kupimwa mimba na shangazi yake na badala yake kumtafuta mwanaume anayehusika na mimba hiyo (Joti)  kuzungumza naye, rejea Suzi anaposema, “Oh Mungu wangu! Nifanye nini sasa? Siwezi kumruhusu shangazi akanipime…oh, nifanye nini mie! Nimtafute Joti, lazima niongee naye.” {Uk. 31}
UJUMBE
Ujumbe ni funzo analolipata fanani anaposoma ama kusikiliza kazi za fasihi, pamoja na ujumbe pia kuna maadili mbalimbali hupatikana, katika tamthiliya hii kuna mafunzo mbalimbali ambayo msomaji wa kazi hii anaweza kuyapata, mafunzo hayo ni kama:
Elimu ya jinsia na ukimwi ni muhimu kwa vijana ili kuwanusuru vijana na mimba za utotoni(mimba zisizotarajiwa) na maambukizi ya virusi vya ukimwi.
Ukimwi hauchagui rika, mwandishi anatupa ujumbe kuwa gonjwa hili la UKIMWI hauchagui mtu, kila mtu anaweza kuupata, kama tunavyoona kwa Fausta na Joti, ni watoto wadogo lakini wanaathirika na virusi vya ukimwi na kusababisha vifo vyao.
Asiyefunzwa na mama yake, hufunzwa na ulimwengu, hili ni funzo linguine tunalilipata katika tamthiliya, mwandishi anatufundisha umuhimu wa wazazi kuwafundishi watoto wao maadili mema na si kuwaacha watoto wakajifunza wenyewe mtaani, wakiwaacha hivyo, huko hujifunza mambo yasiyofaa, tunaona kwa Suzi, Joti, Mwarami, Choggo, Jumbe, wazazi wao hawakuwafundisha elimu ya jinsia na mahusiano watoto wakajifunza wenyewe mambo machafu na hataimaye yakawaletea madhara.
Wazazi ndiyo walimu bora kwa malezi bora na maadili mema kwa watoto wao. Mwandishi anaendelea kutufundisha kuwa, ili vijana wetu wawe na tabia njema, mzazi ni mwalimu bora kabisa anayeweza kumfundisha mtoto wake vema, rejea mwandishi akimtumia muhusika Baba Anna anaposema, “Dunia imeharibika bwana. Mzazi usipomfunza, walimwengu watamfundisha tena sasa si maadili mema bali njia potofu.”
Kinga ni bora kuliko tiba. Ni vizuri jamii ikajikinga na magonjwa mbalimbali, kuliko kutojikinga na baadaye kuanza kutafuta tiba, tiba huwa gharama sana kuliko kujikinga, tunamuona Baba Joti akitumia gharama kubwa kutafuta tiba ya mtoto wake, kama ambavyo mwandisha anasema, “Mtani ushauza rasilimali zako kuuguza mtoto. Ushajitia umskini kwa kuhangaika…” {Uk. 34} Hivyo basi ni vema jamii ikaamua kujikinga dhidi ya matatizo mbalimbali kwani matatizo hayo pindi yanapokukumba huwa ni gharama sana kuyatatua na wakati mwingine matatizo mengine huwa hayana tiba kama tunavyoona katika ugonjwa wa UKIMWI.
Ngono zembe ni chanzo cha maambukizi ya virusi vya ukimwi na mimba zisizotarajiwa, Tunamuona Joti akiambukizwa virusi vya ukimwi kutokana na kushiriki ngono zemba, vilevile tunamuona Suzi akipata mimba na hata kuwa katika wasiwasi wa kuambukizwa virusi vya UKIMWI kutokana na kushiriki ngono zemba. (Rejea ukurasa wa 4 na 34)
MATUMIZI YA LUGHA
Mwandishi ametumia lugha ya kawaida, sentensi fupifupi na inayoeleweka kwa urahisi, pamoja na hayo mwandishi pia ametumia lugha ya kisanaa yenye mbinu mbalimbali za kisanaa kama vile nahau na tamathari za semi.
Matumizi ya methali
“Mzazi usipomfunza, walimwengu watamfundisha.” Uk.
“Shukrani ya punda mateke.” {Uk. 19}
Matumizi ya misemo na nahau
Shoga, mtakatifu wa kwenye mwanga si lazima awe mtakatifu gizani. {Uk. 4}
 “Kakanyaga nyaya.” {Uk. 4}
“Potelea kwao…” uk. 9
“Makapera kibao, mume wangu wa nini. Uk. 7
“Wembamba wa reli treni inapita, uk 6
Kifua simkingii, maana siwi naye. Uk 6
“Kwa mashairi nimekuvulia kofia siku nyingi.” Uk.6
“We pita juu mie nipite chini…”uk 19
 Mbona umetuanika juani. Uk 16
“Hakikisha ndege mjanja ananasa katika tundu bovu.” Uk. 24
(c)  Matumizi ya taswira/lugha ya picha
Dubwana, Manaa yake ni kitu au mtu mwenye umbo kubwa lisilo la kawaida au la hovyo hovyo, mwandishi ametumia neno dubwana kitaswira kuufananisha ugonjwa wa Ukimwi sawa na jambo linalotisha, kuogopesha. (Rejea ukurasa wa 1-2)
Gizani, gizani ni mahali pasipokuwa na mwanga, hivyo mwandishi ametumia neno giza, akimaanisha kukosa maarifa au kutokuwa na ufahamu ya jambo fulani, kwa kifupi kukosa elimu, Rejea mtambaji anaposema, “Kisiwa kizima kipo gizani…watoto ndio kabisa. Wapo katika giza nene.” {Uk. 13}
(d) Matumizi ya tamathali za semi.
Tashibiha,
Hizi ni tamathari ambazo hulinganisha vitu kwa kutumia viunganishi kama, mfano wa, sawa na, mithili ya, kama vile. N.k. baadhi ya tashibiha zinazojitokeza katika tamthiliya hii ni:
“Wewe nawe unakuwa nyuma nyuma Kama koti.” Uk. 4
“Shoga mbona unakuwa mgumu kama mpingo?” uk. 5
“Watu walipukutika, wakapukutika Kama majani ya kiangazi.” Uk.1
“Lile Dubwana limetanda Kama utando wa buibui.” {Uk.13}
 “Miti inayoungua Kama mabua.” Uk. 6
  Sitiari
Hizi ni tamathari za semi ambazo hulinganisha vitu bila kutumia viunganishi, mfano wa tamathali zilizotumika ni pamoja na:
“We mbwa mweusi.” Uk. 8
“Nyoka wee.” Uk.9
 Mjalizo
 Hii ni aina ya tamathali za semi ambazo msanii/mwandishi huitumia kutaja vitu au mambo yaliyo katika orodha bila kutumia viunganishi. Mfano:
“…Lakini soma maneno yake. Yamejaa kejeli, ushari, uchimvi, kusengenyana na kufumbiana mafumbo ya kila aina.” Uk. 6
Nidaa
 Hizi ni tamathali za semi, zinazoonesha hali ya kushangaa au kushangazwa na jambo Fulani, mfano wa tamathali hizi ni:
“Ai, ai, lahaula lakwata…weye, hiki kitoto?” {uk. 9}
 “Oi, oi, oi, toba! Kile si kitoto kama cha kwangu…” {uk.10}
Takriri
Hii ni hali ya kurudiarudia maneno, neno, silabi au sauti zinazolingana katika kazi ya fasihi ili kusisitiza au kutia mkazo jambo fulani. Mfano wa takriri zinazojitokeza katika tamthiliya hii ni:
“Watu walipukutika, wakapukutika Kama majani ya kiangazi.   Wakapukutika.” Uk. 1
 “Waongo! Waongo wakubwa.” Uk. 3
 “Vifo vikawazoa, vikawazoa…vikawazoa.” uk. 2
 “Piga domo, piga doma, nikashinda.” UK. 16
Tanakali sauti
 Hii ni aina ya tamathali ambayo sauti ya kitu fulani huigwa ili kwa lengo la kuburudisha au kuipa dhamira uzito falani. Mfano wa tanakali sauti zilizotumika katika tamthiliya hii ni
“Wacha moyo unipwite pwi,pwi,pwi…” uk.16
Tashititi 
Hii ni aina ya tamathari ya semi ambayo mtu huuliza swali huku jibu lake akilifahamu, mfano wa tashititi zinazojitokea katika tamthiliya hii ni:
“Huyu ni Suzi kweli au nani?” uk.15
MTINDO
Mtindo ni jinsi msanii anavyotumia ufundi, umahiri na hisia zake katika kutenda au kueleza jambo fulani katika kazi ya fasihi, na mtindo ndiyo huweza kumtofautisha msanii/mwandishi mmoja na mwandishi mwingine. Mtindo hutumika kuipamba kazi ya fasihi, baadhi ya mitindo nayotumika katika kazi hii ni pamoja na:


Matumizi ya hadithi ndani ya tamthiliya
Mwandishi ametumia mtindo wa hadithi ambao ni utanzu wa fasihi simulizi ndani ya tamthiliya, mtindo huu unajidhihirisha ukurasa wa kwanza, Mtambaji anapoanza kusimulia hadithi anaposema, “Paukwa” na hadhira inaitikia “Pakawaaaaaaa” na Mtambaji anaendelea, “Hapo zamani za kale paliondokea kisiwa kimoja…” {Uk. 1} Ni utanzu wa hadithi pekee ndiyo huwa na mwanzo wa namna hiyo.
Matumizi ya wimbo/shairi ndani ya tamthiliya
Mwandishi pia ametumia wimbo kuipamba kazi yake, wimbo unajitokeza ukurasa wa 27 Anna anaimba wimbo unaowataka wanaume wanaomtaka kimapenzi kuacha kumfuatafuata, muda wake wa kujihusisha na mahusiano ya kimapenzi haujafika bado mwanafunzi.
        “Anna Anna Anna mie niacheni mie x2
          Msichana mdogo bado nasoma niacheni mie.
          Muda wangu kufanya hayo haujafika mie.
             Pesa zenu, na lifti zenu niacheni mie.
              Anna Anna Anna mie niacheni x2”
Matumizi ya lugha ya majibizano/dialojia na masilmulizi
Kama ilivyo ada, mtindo wa lugha unaotumika katika tamthiliya, kwa asilimia huwa ni mtindo wa majibizano, yaani dialojia. Hivyo basi hata katika tamthiliya hii, mwandishi kwa kiasi kikubwa ametumia mtindo wa majibizano na kidogo ametumia masimulizi, (Rejea masimulizi ya Mtambaji ukurasa wa 1-2, 3-4, na 36)
 Matumizi ya nafsi zote tatu
Pia nafsi zote tatu zinajitokeza katika tamthiliya hii,
Nafsi ya kwanza, mfano, Mimi nawashangaa… {Uk. 6} Najua litamuuma tu (uk.7), Tumebomoa ghala imara…” {Uk. 6}
Nafsi ya pili, mfano, “Utamaliza kanga zilizoandikwa kila aina ya maneno…” Wewe unamwona Fausta alikuwa mdogo?
Nafsi ya tatu, mfano …alikufa kwa ukimwi” uk. 9, atakutafuta tu mwenyewe.” (uk 17), “Wanashindwa kutofautisha kati ya puto na kondomu.” (Uk. 13)
MUUNDO
Muundo ni mfuatano wa masimulizi au visa katika kazi ya sanaa ya fasihi, hivyo basi.muundo wa tamthiliya hii ni wa moja kwa moja, yaani visa vyake vimepangwa kuanzia kisa cha kwanza, kati hadi mwisho, katika kuvipanga visa vyake, mwandishi ameigawa kazi yake katika sehemu sita, ambazo amezipa majina, Sehemu ya kwanza, Sehemu ya Pili, ya Tatu, ya Nne, Tano na Sehemu ya Sita.
Sehemu ya kwanza.
Mtambaji anasimulia habari za Dubwana (Ukimwi), anasimulia namna wakubwa wanavyoelimishana namna ya kujilinda na ugonjwa huo, huku wakiwaacha watoto wakiangamia kwa kukosa elimu ya jinsia na ukimwi.
Sehemu ya Pili
Hapa mwandishi anatuonesha nyumbani kwa Mama Suzi, Mama Suzi na Mama Joti wanapeana habari za kifo cha Fausta kilichosababishwa na ukimwi, Mama Suzi anakuta kasha la vidonge kwenye mfuko wa sketi ya Suzi wakati akifua jambo linalozua mgogoro kati ya Suzi na mama yake, Mjomba na Baba Anna wanamshauri Mama Suzi kuacha kutumia ukali na badala yake anatakiwa kumpa elimu ya jinsia binti yake ili ajitambue jambo linalopingwa vikali na Mama Suzi.
Sehemu ya Tatu
Hapa mwandishi anatuonesha mtaani, Joti anakutana na Suzi, Suzi anaamua kuachana na Joti kwa sababu ya vidonge vya kuzia mimba alivyopewa na Joti kumsababishia kupigwa na mama yake. Joti anawasimulia wenzake namna alivyofanikiwa kumpata Suzi, Joti, Jumbe, Choggo na Mwarami wanaenda mtaani kuangalia sinema za X.
Sehemu ya Nne
Tukio linatendeka njiani, Joti na Suzi wanakutana, Suzi anamlaumu Joti kwa kuwa na mahusiano ya kimapenzi na wasichana wengine, wanaamua kurudisha uhusiano wao, Joti anaanza kujisikia vibaya, Jumbe anaamua kumpeleka nyumbani, Mwarami anaonekana akimshawishi Anna amkubalie ombi lake la kuanzisha mahusiano ya kimapenzi, Anna anaonesha msimamo anamkatalia, mwandishi pia anatuonesha namna Anna anavyoshinda vishawishi vya kingono.
Sehemu ya Tano
Tukio linatendeka chumbani kwa Suzi akiwa na Anna, Suzi anajisikia vibaya, anahisi huenda ana mimba, anataka kuitoa, rafiki yake Anna anamshauri kuachana na mpango huo kwani ni hatari, anaamua kwenda kwa Joti kuzungumza naye suala hilo.
Sehemu ya Sita
Hii ni sehemu ya mwisho, mwandishi anatuonesha nyumbani kwa Baba Joti, tunaona namna Baba Joti alivyoangaika kwa waganga mbalimbali kutafuta tiba ya Joti bila mafanikio, mwisho wanaamua kumpeleka hospitali, huko wanapata wajibu kuwa Joti amethirika na virusi vya ukimwi, Jirani anamshauri Baba Joti kumpeleka Joti kwa mganga mwingine, Mjomba anamshauri Baba Joti kuachana na mpango huo kwani ugonjwa alionao Joti hauna tiba wala dawa. Suzi anawasili kwa akina Joti anagundua Joti ana ukimwi, Joti anafariki dunia, Suzi anakuwa na wasiwasi kama naye atakuwa ameambukizwa virusi vya ukimwi, anabaki akijutia kwa kukosa elimu ya jinsia na ukimwi.  Na mchezo unaishia hapo.
MANDHARI
Mandhari ni sehemu au eneo ambalo visa na matukio hutendeka katika kazi ya fasihi, katika kazi ya fasihi mandhari huweza kuwa mandhari halisi au ya kubuni, katika tamthiliya mwandishi ametumia mandhari ya kubuni, hivyo basi, mandhari ya tamthiliya hii yanaweza kuwa sehemu yoyote ile katika nchi za Kiafrika. Pia mwandishi anatuonesha visa na matukio yakitendeka mandhari ya nyumbani, mtaani, njiani n.k.
Mandhari ya nyumba
Katika mandhari ya nyumbani, tunaona nyumbani kwa Mama Suzi na Nyumbani kwa Baba Joti, kwa Mama Suzi tunaona ukuta uliowekwa kati ya mzazi na mtoto kuhusu elimu ya jinsia kwa mtoto, Mama Suzi anamuadhibu Suzi kwa kukuta vidonge vya kuzuia mimba kwenye mfuko wa sketi ya Suzi, Suzi anaanza kujisikia vibaya, anafikiria kuitoa mimba. Nyumbani kwa Baba Joti, tunaona kuumwa kwa Joti, kugundulika kuwa ana ukimwi na kufariki kwake.
Hivyo mwandishi ametumia mandhari hii, ili kufikisha dhamira ya umuhimu wa elimu ya jinsia kwa watoto, malezi bora ya mtoto, tatizo la ugonjwa wa ukimwi na athari zake katika familia, n.k.
Mandhari ya Mtaani
Katika mandhari haya, mwandishi, anatuonesha Joti na Suzi wakiwa katika mazungumzo ya uhusiano wao wa kimapenzi, pia tunaoneshwa kuwa ni mahali ambapo Joti na wenzake hukutana na kupanga mambo yao ya mapenzi. Mwandishi anatumia mandhari haya, kuonesha namna watoto wanavyoharibikiwa kitabia mtaani, mandhari ya njiani inatuonesha namna watoto wakike wanavyosumbuliwa na wanaume wasiokuwa waadilifu ambao huwataka kimapenzi.
FALSAFA YA MWANDISHI
Falsafa ni mchujo wa mawazo ya mwandishi kuhusu maisha na jamii yake. Falsafa ya mwandishi wa tamthilia hii anaamini kuwa, ili jamii yoyote ile iweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii husika, elimu ni nyenzo muhimu sana ya kupambana na changamoto hizo. Na elimu hiyo isitolewe kimatabaka.
MTAZAMO WA MWANDISHI
Mwandishi ana mtazamo wa kiyakinifu, ana mtazamo kuwa, matatizo yote yanayotokea katika jamii chanzo ni jamii yenyewe na jamii yenyewe ndiyo inayotakiwa kukabiliana na matatizo hayo, na ndiyo maana anaitaka jamii yake ibadilike.
MSIMAMO WA MWANDISHI
Mwandishi ana msimamo wa kimapinduzi, kwani anaitaka jamii yake ibadilike ili kuendana na wakati, na anaitaka jamii kuachana na mila na desturi zilizopitwa na wakati ili kukabiliana na changamoto zinazoikabili jamii.
JINA LA KITABU
Jina la kitabu au tamthiliya hii ni Kilio Chetu,kilio chetu ina maana ya tatizo, balaa au janga linapoingia katika jamii ni letu sisi sote. Hivyo basi, jina la kitabu Kilio Chetu linasadifu sana yaliyomo katika tamthiliya hii. Tukianza na:
Tatizo la ukimwi
Mwandishi anajadili ukimwi kuwa ni ugonjwa hatari sana, ni ugonjwa usiobagua mkubwa wala mtoto, kama mwandishi anavyosema, “Ukimwi hauchagui mkuwa wala mdogo.” {Uk. 25} hii inathibitisha kuwa tatizo hili la ukimwi ni letu sote tunatakiwa wote kupambana nalo, na hapa ndipo linapokuja suala la Kilio Chetu.
Elimu ya jinsia
Mwandishi pia anaonesha kuwa suala la watoto/vijana kupewa elimu ya jinsia na ukimwi ni kilio cha jamii, jamii inasisitiza na kupigia kelele suala la vijana kupewa elimu ya jinsia na ukimwi, kwa mfano, mwandishi anamtumia muhusika Baba Anna anaposema, “Mimi bwana nitaendelea kusisitiza juu ya elimu hii.” Mwandishi anaendelea kwa kusema akimtumia muhusika Mjomba, “Tutaendelea kuwaelimisha wazazi umuhimu wa elimu hii.” {Uk.12} Hivyo tunaona kuwa Baba Anna na Mjomba wanatoa kilio chao cha kutaka watoto kuelimishwa elimu ya jinsia.
KUFAULU NA KUTOFAULU KWA MWANDISHI
(A)  KUFAULU KWA MWANDISHI.
Hapa tunaangalia kufanikiwa kwa mwandishi katika vipengele vya fani na maudhui, Kifani mwandishi amefanikiwa sana, tukianza na:
Mwandishi amefanikiwa kuwajenga wahusika wake vizuri, amewajenga wahusika katika rika tofauti tofauti na kila rika amefanikiwa kuwavisha uhusika unaendana na rika husika, na amafanikiwa kuonesha namna kila rika linavyoweza kuathiliwa na UKIMWI na kuitaka jamii kutoa elimu ya jinsia kwa kila rika.
Mwandishi amefanikiwa kuifanyanga lugha yake kiufundi, amefanikiwa kutumia lugha nyepesi inayoeleweka na kila mtu inayoambatana na matumizi ya methali, misemo/nahau na tamathali za semi, matumizi yote haya ya lugha yamesaidia kwa kiasi kikubwa kufikisha ujumbe uliokusudiwa na kuipamba kazi husika. (Rejea kipengele cha Matumizi ya lugha)
Katika suala la mtindo, mwandishi amefanikiwa kwa kiasi kikubwa sana, kwani amefanikiwa kutumia utanzu wa hadithi na wimbo kuipamba kazi yake na ikawa kazi ya kuvutia na inayovuta hisia za msomaji kupenda kuendelea kukisoma kitabu hiki zaidi na zaidi. (Rejea kipengele cha Mtindo)
Mwandishi ametumia muundo rahisi, muundo unaeleweka kwa urahisi na hivyo kumsaidia mwandishi kufikisha ujumbe alioukusudia kwa jamii husika, visa vyake amevipangalia vizuri hali inayomfanya msomaji apende kuendelea kukisoma kitabu hiki ukurasa mmoja hadi mwingine hadi anakimaliza kitabu hiki.
Kwa upande wa maudhui, mwandishi amefanikiwa kuonesha dhamira mbalimbali ambazo kwa kiasi kikubwa zina uhalisia katika jamii yetu. (Rejea dhamira)
Vilevile, kwa upande wa ujumbe, mwandishi  amefanikiwa kutupa ujumbe au mafunzo muhimu sana ambayo kama jamii itayazingatia basi mafunzo haya yanaweza kuwasaidia sana. (Rejea Kipengele cha ujumbe)
Migogoro, mwandishi amefanikiwa kuibua migogoro, kuonesha chanzo, upeo na hata baadhi ya migogoro amefanikiwa kuitolea suluhisho. (rejea kipengele cha Migogoro)
KUTOFAULU KWA MWANDISHI
Mwandishi ameshindwa kutuonesha mwanamke aliyemuambukiza Joti virusi vya UKIMWI.
Mwandishi pia ameshindwa kutuonesha hatima ya akina Jumbe na Choggo kama nao waliathirika na UKIMWI au la, maana hawa wote matendo yao alikuwa yanafanana tu na Joti.
Mwandishi ameshindwa kutuambia alipo baba yake, kama amesafiri au amefariki.

Maswali ya vitabu na majibu yake

 NECTA 2012 “Washairi ni wataalamu wazuri na waliobobea katika kutumia taswira zinazotoa ujumbe kwa jamii.” Tumia taswira tatu kwa kila diwa...